Dkt Mwigulu aagiza ujenzi wa viwanja vya mazoezi AFCON vijengwe


WAZIRI MKUU, Dkt. Mwigulu Nchemba ameagiza kuongezwa kasi ya ujenzi wa viwanja vya mazoezi vitakavyotumika katika mashindano ya Kombe la Mataifa ya Afrika (AFCON) 2027, ili vikamilike kwa wakati na kukidhi viwango vinavyotakiwa na Shirikisho la Mpira wa Miguu Afrika (CAF).

Amesema kazi hiyo inapaswa kufanyika kwa kasi, ikiwemo kuongeza muda wa kufanya kazi pale inapobidi, ili viwanja vikamilike kwa wakati na Tanzania iwe tayari kabla ya ukaguzi wa maandalizi unaotarajiwa kufanywa na CAF.

Waziri Mkuu ametoa maelekezo hayo leo (Ijumaa, Agosti 21, 2026) baada ya kukagua maendeleo ya ujenzi wa viwanja vya mazoezi vya Farasi na Leaders Club jijini Dar es Salaam, ambavyo ni miongoni mwa viwanja vitakavyotumika katika maandalizi ya mashindano ya AFCON 2027 yatakayofanyika kwa ushirikiano wa Tanzania, Kenya na Uganda.

Amesema Tanzania haipaswi kusubiri hadi dakika za mwisho kukamilisha maandalizi yake kwa sababu CAF inahitaji kujiridhisha mapema kuwa miundombinu inayohitajika iko tayari.

“Twendeni tufanye kazi usiku na mchana tumalizie asilimia iliyosalia. Wenzetu wanaosimamia mashindano hawawezi kurisk tu kwamba tuko tayari, wanataka wajionee kwamba tuko tayari kukiwa bado kuna muda wa kutosha,” amesema.

Dkt. Mwigulu amesema mashindano ya AFCON hayapaswi kutazamwa kama tukio la michezo pekee, bali ni fursa kubwa ya kiuchumi ambayo Tanzania inapaswa kujiandaa kuitumia kikamilifu.

“Hii si michezo tu, bali pana uchumi ndani yake,” amesema na kuongeza kuwa baada ya kukamilisha miundombinu, nchi inapaswa kuelekeza nguvu katika kujiandaa kimkakati ili kunufaika na fursa za kiuchumi zitakazoambatana na mashindano hayo.

Katika ukaguzi huo, Waziri Mkuu pia ametoa maelekezo ya kushughulikia malalamiko ya wafanyakazi wanaoshiriki ujenzi wa viwanja hivyo, hususan kuhusu mikataba ya ajira, malipo ya muda wa ziada na stahiki nyingine.




Machapisho maarufu kutoka blogu hii

FIFA yatoa orodha ya vilabu bora duniani, Simba na Yanga zachuana vikali

Kocha Simba anataka wachezaji wapya watano

HISTORIA YA TIMU YA MASHUJAA YA KIGOMA, KUMBE NI SHEA YA JESHI NA WANANCHI