Makamu wa Rais Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi, ametembelea na kukagua maendeleo ya ujenzi wa Uwanja wa Arusha, utakaotumika katika fainali za AFCON 2027, unaojengwa jijini Arusha. Dkt. Nchimbi amepongeza maendeleo ya ujenzi wa uwanja huo, ambapo amesema ni faraja kuona ahadi ya Rais Samia Suluhu Hassan aliyoitoa ili kuvutia michuano hiyo kufanyika nchini Tanzania, inatakelezwa kikamilifu. Makamu wa Rais amemshukuru Rais kwa kuendelea kutoa fedha ili kuhakikisha uwanja huo unakamilika kwa wakati. Dkt. Nchimbi ameishukuru Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo pamoja na mkoa wa Arusha, wakandarasi na mshauri Elekezi kwa kazi waliyofanya katika Uwanja huo. Makamu wa Rais amewataka viongozi wa wizara pamoja na Mkoa wa Arusha kusimamia vema agizo la Rais Samia Suluhu Hassan la kuhakikisha barabara zinazotumika katika kufika uwanjani hapo zinakamilika kwa wakati.