Machapisho

Depu mbioni kwenda Petro de Luanda

Picha
Taarifa za ndani zinaeleza kuwa klabu ya Petro de Luanda ya Angola imepiga hatua kubwa katika harakati za kumsajili mshambuliaji wa Young Africans, Aurélio Depu (26). Inaelezwa kuwa klabu hiyo imeweka mezani kiasi cha takribani KZ milioni 455 (sawa na karibu Shilingi bilioni 1.3 za Kitanzania) ili kufanikisha usajili wa nyota huyo. Mbali na ada ya usajili, Petro de Luanda inadaiwa kumpatia Depu mkataba wa miaka miwili wenye kipengele cha kuongeza mwaka mmoja zaidi endapo pande zote zitaridhishwa na utendaji wake. Vyanzo vinaongeza kuwa hakuna tofauti kuhusu maslahi binafsi kati ya mchezaji huyo na Petro de Luanda, huku Young Africans ikionekana kuwa tayari kusikiliza ofa kwa ajili ya kumruhusu kuondoka. Iwapo dili hilo litakamilika, Aurélio Depu anatarajiwa kuwa mchezaji anayelipwa mshahara mkubwa zaidi ndani ya kikosi cha Petro de Luanda. Depu anampisha beki kisiki aliye tambulishwa leo Bukombe GEITA Komara kutoka Ivory coast.

Gor Mahia yatangulia fainali Kagame Cup

Picha
Timu ya Gor Mahia ya Kenya imefanikiwa kutinga fainali ya michuano ya Kagame Cup baada ya kuifunga Al Hilal ya Sudan mabao 8-7 kufuatia sare ya 1-1 uwanja wa Amahoro jijini Kigali Rwanda. Magoli yote yamefungwa na wachezaji wa Al Hilal ambapo Steven Ebuela amejifunga na Ansumana Samura akasawazisha.

Clatous Chama atangaza kustaafu

Picha
Mwamba wa Lusaka, Clatous Chota Chama, ametangaza rasmi kustaafu kuchezea Timu ya Taifa ya Zambia Chipolopolo, akihitimisha safari yake ndefu na ya mafanikio katika soka la kimataifa. Chama, ambaye kwa sasa yupo nchini Rwanda na kikosi cha Simba SC kwa ajili ya kambi ya maandalizi ya msimu mpya, amebainisha kuwa umefika wakati sahihi wa kutundika daluga katika ngazi ya taifa na kuweka umakini wake wote kwenye soka la klabu.

Injinia Hersi amkabidhi jezi mbunge wa Bukombe

Picha
Rais wa Klabu ya Yanga SC, Eng. Hersi Said, akimkabidhi jezi Mbunge wa Jimbo la Bukombe na Naibu Waziri Mkuu Mstaafu, Dkt. Doto Biteko zoezi lililofanyika katika Uwanja wa Bukombe kwenye uzinduzi wa Wiki ya Mwananchi 2026. Yanga SC ipo Ushirombo, Wilaya ya Bukombe Mkoa wa Geita kwa ajili ya uzinduzi na maadhimisho ya Wiki ya Mwananchi ikiwa ni kwa mara ya kwanza kihistoria kwa tamasha hilo kufanyika nje ya mkoa wa Dar es Salaam.

Doumbia aendelea kucheka na nyavu, ikiiua El Marreikh 2-0

Picha
Klabu ya Simba imeibuka na ushindi wa mabao 2-0 dhidi ya El Merreikh ya Sudan katika mchezo wa kirafiki uliochezwa Kigali, Rwanda. Simba imepata mabao yake kupitia kwa Libasse Gueye aliyefunga bao la kwanza, kabla ya Ibrahim Doumbia kuongeza la pili na kuipa timu hiyo ushindi. Hii ni mara ya pili kwa straika huyo mpya wa Simba kucheka na nyavu ambapo mara ya kwanza alitupia wakati Simba ilipocheza na Singida BS kwenye Kagame CECAFA Cup

Simba yasimama kwa muda

Picha
Klabu ya Simba imetangaza kusimamisha kwa muda masuala yote yaliyokuwa yakiendelea kuhusu Baraza la Wadhamini, kufuatia uamuzi uliofikiwa katika kikao cha Bodi ya Wakurugenzi kilichofanyika Agosti 3, 2026. Kupitia taarifa iliyotolewa leo Agosti 4, 2026 Bodi imeeleza kuwa imeamua kusimamisha matukio yote yaliyotokea awali kuhusiana na Baraza la Wadhamini hadi itakapotolewa taarifa nyingine. Katika kipindi hicho, Bodi imesema itaelekeza nguvu zake katika masuala muhimu yanayohusu klabu, ikiwemo mchakato wa usajili wa Wachezaji, maandalizi ya Simba Day, mchezo wa Ngao ya Jamii pamoja na maandalizi ya Ligi Kuu ya Tanzania Bara kwa msimu ujao. Aidha, Bodi imewasihi Wanachama na wapenzi wa Simba kuendelea kuiunga mkono klabu hiyo ili kuhakikisha inapata mafanikio makubwa katika msimu unaotarajiwa kuanza hivi karibuni. Taarifa hiyo imesainiwa na Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi wa Simba, Crescentius Magori pamoja na Makamu Mwenyekiti wa Bodi, Murtaza Mangungu.

Yanga yatambulisha beki wa kati mpya

Picha
Klabu ya Yanga SC imemtambulisha beki wa kati, Oumar Farouk Komara kama mchezaji mpya klabuni hapo baada ya kukamilisha uhamisho wake kutoka klabu ya Golden Arrows ya Nchini Afrika Kusini. Komara 25, raia wa Ivory Coast ambaye pia ana uwezo wa kucheza kama Kiungo Mkabaji tayari yupo Geita na Kikosi cha Yanga na ujio wake unalenga kuongeza kuimarisha zaidi safu ya ulinzi na viungo wa Yanga kuelekea msimu mpya wa mashindano.