Mahakama Kuu ya Tanzania imeipa ushindi Azam Media Limited katika kesi ya madai ya haki miliki iliyofunguliwa na bondia Amosi Mwamakula.
Awali, Mahakama ya Kinondoni iliiamuru Azam Media Limited kumlipa bondia huyo kiasi cha shilingi milioni 250, baada ya kudai kuwa kampuni hiyo ilichukua wazo lake la kipindi cha “Boxing Kazi Kazi” kinachohusu masuala ya ndondi na kukitumia kwa jina la “Vitasa”.
Hata hivyo, Mahakama Kuu baada ya kusikiliza shauri hilo imeipa ushindi Azam Media Limited kwa kuzingatia sheria za hati miliki.
Wakili Neema Mbaga anayewakilisha Azam Media, amesema ushindi huo unaiwezesha Azam TV kuendelea na shughuli zake za kurusha vipindi vinavyohusiana na ndondi na mapambano mubashara ya ndondi.