Maelfu wamzika Papa Francis

KIONGOZI wa Kanisa Katoliki, na Rais wa Vatican, Papa Francis amezikwa katika Kanisa kuu la Santa Maria Maggiore mjini Roma baada ya ibada ya mazishi iliyohudhuriwa na watu 250,000 katika uwanja wa St. Peter’s mjini Vatican.

Mbali na viongozi wa Dunia, hafla ya mazishi ya Papa Francis imehudhuriwa Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Philip Isdor Mpango ambaye aliambatana na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Mahmoud Kombo pamoja na watu muhimu kama vile Rais wa Marekani Donald Trump, Rais wa Ufaransa Emmanuel Macron na Waziri Mkuu wa Uingereza, Keir Starmer.

Sherehe za mazishi zilianza saa 5:00 asubuhi kwa saa za Afrika Mashariki, huku mwili wa Papa Francis ukibebwa kwenye uwanja wa Kanisa kuu la Mtakatifu Petro ambapo baada ya sherehe hizo, Kardinali Giovanni Battista Re alitoa hotuba akisisitiza uhusiano wa Papa na watu na umuhimu anaoupa kwa amani huku akinukuu maneno ya Papa, “Jenga madaraja, sio kuta.”

Baada ya sherehe, mwili wa Papa Francis ulihamishiwa kwenye Kanisa kuu la Santa Maria Maggiore la Roma ambapo amezikwa kwenye kaburi lake lenye jina “Franciscus”.

Papa Francis amekuwa Papa wa kwanza tangu mwaka 1903 kuzikwa nje ya Vatican na anakuwa Papa wa 8 kuzikwa katika Basilica ya Santa Maria Maggiore tangu mwaka 1669. Papa Francisko amekuwa na desturi ya kusali katika Kanisa Kuu la Santa Maria Maggiore wakati wa kila ziara yake nje ya Roma.