Ruka hadi kwenye maudhui makuu

Barca watwaa ufalme wa Uhispania



Barcelona ndio wafalme wa Uhispania baada ya kuinua taji lao la tano katika miaka saba la La Liga Jumapili walipowarudishia watetezi Atletico Madrid mkono kwa kuwachapa goli moja kwa yai ugani Vincente Calderon.

Wana Blaugrana walipoteza kombe hilo musimu jana baada ya kupokea kichapo cha 1-0 uwanjani mwao Nou Camp katika mechi ya kufunga kampeni lakini walipata kisasi na kutamba kukamilisha taji la 23 katika historia yao ya kifahari.

Bila shaka, nyota wao shupavu, Leo Messi wa Argentina ndiye aliyeitikia mwito na kuzamisha goli maridadi kama ilivyo kawaida yake kuamua kivumbi hicho kilichowaniwa kwa makali katika dakika ya 65 kipindi cha pili.


Staa huyo alipokea mpira nje ya kisanduku na kumlisha ngozi mshambuliaji Pedro ambaye hakusita kumrudishia tena ndani ya eneo la hatari na baada ya kucheza densi na walinda ngome wawili, alilenga kombora la chini lilioishia kizimbani.

Mwenzake maarufu, Neymar wa Brazil, nusura ahakikishie Barca utawala lakini akanoa shabaha kwa ncha ya unywele dakika sita baadaye huku kipa Carlos Bravo akiokoa kimiujiza simiti kali kutoka nje ya kisanduku ikisalia dakika tatu muda wa kawaida kutimia.

Barca walipata nafasi ya mwisho kutia kimyani lakini kipa wa Atletico Oblak aliuondoa kwa ustadi mkubwa mkwaju wa adhabu wa Messi.

Sintofahamu ilitanda katika muda wa dakika tatu za maongezi wakati Neymar alilishwa kadi ya njano kwa kupoteza muda huku wakirushiana maneno makali na Diego Godin, shujaa aliyefungia Atletico bao la ushindi musimu jana camp Nou.

Baada ya wawili hao kutenganishwa huku Neymar akimhepa beki huyo aliyeonekana kupandwa na mori, utawala wa Atletico kama mabingwa wa Uhispania ulimalizwa na kipenga cha mwisho.

Wachezaji wa Barca walibaki uwanjani wakisherehekea ushindi wao, huku viungo walioumia kama vile nyota Luis Suarez na beki Thomas Vermaelen wakiungana nao kuimba kwa bwembwe na vifijo.
Taji hilo ni la kwanza tangu kwa nahodha wao wa zamani, Luis Enrique, ambaye alitwaa utawala wa miamba hao mwishoni mwa musimu jana huku akisalia kuongoza Barca katika fainali za kombe la Copa del Rey na lile la thamani kubwa, Ligi ya Mabingwa Ulaya.

Barca walipanda hadi alama 93, nne mbele ya waasimu wao wakuu Real Madrid ambao waliongozwa na magoli matatu kutoka nyota wao na mchezaji bora zaidi duniani, Cristiano Ronaldo kubomoa wenyeji Espanyol 4-1 katika kivumbi kilicho chezwa sambamba na hiki.

Hima yao iliambulia patupu kwani ikisalia mkondo wa mwisho shindano hilo kukatika wiki ijayo, hakuna anaweza kushika Barca.

Machapisho maarufu kutoka blogu hii

FIFA yatoa orodha ya vilabu bora duniani, Simba na Yanga zachuana vikali

SHIRIKISHO la Soka Afrika (CAF) limetoa orodha ya viwango vya ubora wa klabu barani, Simba ikiendelea kuwa juu ya klabu nyingine za Tanzania, nafasi ya tano. Orodha hiyo imetoka leo kuelekea droo ya hatua za awali za michuano ya klabu Afrika ambayo kwa mara ya kwanza kihistoria itafanyika nchini katika studio za Azam Tv, Tabata Jijini Dar es Salaam. Yanga ambayo kama Simba itashiriki Ligi ya Mabingwa — yenyewe inashika nafasi ya 12, wakati timu nyingine katika orodha hiyo ni Namungo FC wanaoshika nafasi ya mwisho, ya 75 kwa pamoja na Salitas FC ya Burkina Faso, Ahli Benghazi ya Libya na NAPSA Stars ya Zambia. Kwa msimu ujao mbali na Simba na Yanga kushiriki Ligi ya Mabingwa, Azam FC na Singida Black Stars zitashiriki michuano ya Kombe la Shirikisho Afrika.

HISTORIA YA TIMU YA MASHUJAA YA KIGOMA, KUMBE NI SHEA YA JESHI NA WANANCHI

Timu inaitwa Mashujaa Lake Tanganyika FC ( Mashujaa FC ) ilianza rasmi kampeni yake ya kupanda Ligi Kuu tarehe 29/9/2018 na imepanda Ligi Kuu 25/06/2023 miaka mitano ya kupambana kwenye Ligi Daraja la kwanza Championship. Timu hii inaendeshwa kwa ushirikiano wa pande mbili kati ya Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) na Halmashauri ya Manispaa ya Kigoma Ujiji kwa niaba ya Wananchi wa Kigoma. Muelewe hapa maana wengi wanasema ni timu ya Jeshi asilimia 100% Nembo ya timu ni Sokwe Dume, Shujaa wa Hifadhi za Gombe na Mahale zilizopo mkoani Kigoma. Rangi ya kwanza ya jezi ya timu (first kit) ni hiyo hapo chini na kwenye nembo ya timu ni rangi za tunda la michikichi (mawese ). Hii kama njano ni mawese yaliyoganda na huo wekundu ni mawese ya moto. Ukishika tunda la Mse juu utaona wekundu na ukikata katikati utaona njano. Nyeupe ni ‘nazi’ ya Mse hizi ni alama za utajiri wa Kigoma Jezi nyingine ni blue inayowakilisha Ziwa Tanganyika na Jezi nyingine ni Nyeupe

Beno Ngassa mdogo wa Mrisho Ngassa anayekipiga Tanzania Prisons

Miongoni mwa viungo wa pembeni wanaofanya vizuri ni Benodict Khalfan Ngassa ambaye amekuwa akifanya vizuri. Ngassa ambaye ni mtoto wa mchezaji wa zamani wa Pamba Jiji na Simba SC, Khalfan Ngassa, pia ni mdogo wa kiungo mshambuliaji wa zamani wa Yanga, Simba na Azam, Mrisho Ngassa anatajwa ni mmoja kati ya wachezaji wanaotazamiwa kufanya makubwa siku za usoni. Mambo Uwanjani Blog itawaletea Makala maalum ya kiungo huyo hatari ambaye ndoto zake ni kufuata nyayo za kaka yake Mrisho Ngassa. Beno Ngassa