Ruka hadi kwenye maudhui makuu

KILI STARS YATUA SALAMA NAIROBI.

BAADA ya safari ya takriban saa nne angani, hatimaye timu ya soka ya taifa ya Bara, Kilimanjaro Stars imeatua salama Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Jomo Kenyatta mjini Nairobi, Kenya tayari kuwania taji la nne la Kombe la Mataifa ya Afrika Mashariki na Kati, CECAFA Challenge.

Katika michuano hiyo inayoanza kutimua vumbi Novemba keshokutwa, Stars imepangwa Kundi B pamoja na Zambia, Burundi na Somalia na itafungua dimba na Chipolopolo Alhamisi Uwanja wa Machakos.

Stars imetua hapa saa 2:45 usiku baada ya safari ndefu kidogo wakipitia Kigali, Rwanda kabla ya kutua Nairobi na iliwachukua saa nzima hadi kupanda basi kuelekea hotelini baada ya kukamilisha taratibu za kuingia nchini hapa za Idara ya Uhamiaji.

Stars iliagwa jana mchana kwa hafla fupi kambini kwao katika hoteli ya Accomondia jijini Dar es Salaam na kukabidhiwa bendera na Katibu wa Baraza la Michezo la Taifa (BMT), Henry Lihaya.

Katika hafla hiyo, kocha wa Stars, Mdenmark Poulsen pamoja na kumtaja beki Kevin Yondan kuwa Nahodha mpya, pia amesema kwamba lengo moja kubwa kupigana kukata tiketi ya kucheza Robo Fainali kutoka kwenye Kundi lao B, na baada ya hapo mapambano mengine yatafuatia.


Amesema anafurahi wachezaji wake wako tayari sana kwa ajili ya mashindano hayo na wamemuahidi kufanya vizuri.

Nahodha mpya, Yondan kwa upande wake alisema kwamba amefurahia wadhifa huo na kwa pamoja na wachezaji wenzake, wanaahidi kwenda kupigana kurejesha heshima ya timu yao iliyopotea kwa sasa.

“Tunaahidi kwenda kupigana na Mungu atatujaalia tutarudi na Kombe na kurudisha heshima yetu, kwa sababu timu yetu kwa sasa  ni kama imeshuka hivi na kupoteza heshima yake mbele ya wananchi, ila tukirudi na Kombe hapa, heshima itarudi,”alisema.

Mkuu wa Msafara wa Stars iliyotwaa Kombe la Challenge mara tatu, 1974, 1994 na 2010, Geoffrey Nyange ‘Kaburu’ alisema wanakwenda Nairobi, Kenya kupigana kwa nguvu zote kuhakikisha Kombe la Challenge linakuja Dar es Salaam.

Wachezaji walitua na Stars hapa ni makipa Deogratius Munishi (Yanga), Ivo Mapunda (Gor Mahia, Kenya) na Aishi Manula (Azam). Mabeki ni Erasto Nyoni (Azam), Himid Mao (Azam), Ismail Gambo (Azam), Kelvin Yondani (Yanga), Michael Pius (Ruvu Shooting) na Said Moradi (Azam).

Viungo ni Amri Kiemba (Simba), Athuman Idd (Yanga), Frank Domayo (Yanga), Haruna Chanongo (Simba), Hassan Dilunga (Ruvu Shooting), Ramadhan Singano (Simba) na Salum Abubakar (Azam) na washambuliaji Elias Maguli (Ruvu Shooting), Faridi Musa (Azam), Joseph Kimwaga (Azam), Juma Liuzio (Mtibwa Sugar) na Mrisho Ngasa (Yanga).

Washambuliaji Mbwana Samata na Thomas Ulimwengu wa TP Mazembe ya DRC watajiunga na timu hiyo jijini Nairobi, Desemba 1 mwaka huu wakitokea Lubumbashi ambapo Novemba 30 mwaka huu TP Mazembe itacheza fainali ya Kombe la Shirikisho Afrika.

Benchi la Ufundi la timu hiyo linawajumuisha Kim Poulsen (Kocha Mkuu), Sylvester Marsh (Kocha Msaidizi), Juma Pondamali (Kocha wa Makipa), Leopold Tasso (Meneja wa Timu), Dk Mwanandi Mwankemwa (Daktari wa Timu), Frank Mhonda (mtaalamu wa tibamaungo) na Alfred Chimela (Mtunza Vifaa).

Machapisho maarufu kutoka blogu hii

FIFA yatoa orodha ya vilabu bora duniani, Simba na Yanga zachuana vikali

SHIRIKISHO la Soka Afrika (CAF) limetoa orodha ya viwango vya ubora wa klabu barani, Simba ikiendelea kuwa juu ya klabu nyingine za Tanzania, nafasi ya tano. Orodha hiyo imetoka leo kuelekea droo ya hatua za awali za michuano ya klabu Afrika ambayo kwa mara ya kwanza kihistoria itafanyika nchini katika studio za Azam Tv, Tabata Jijini Dar es Salaam. Yanga ambayo kama Simba itashiriki Ligi ya Mabingwa — yenyewe inashika nafasi ya 12, wakati timu nyingine katika orodha hiyo ni Namungo FC wanaoshika nafasi ya mwisho, ya 75 kwa pamoja na Salitas FC ya Burkina Faso, Ahli Benghazi ya Libya na NAPSA Stars ya Zambia. Kwa msimu ujao mbali na Simba na Yanga kushiriki Ligi ya Mabingwa, Azam FC na Singida Black Stars zitashiriki michuano ya Kombe la Shirikisho Afrika.

Beno Ngassa mdogo wa Mrisho Ngassa anayekipiga Tanzania Prisons

Miongoni mwa viungo wa pembeni wanaofanya vizuri ni Benodict Khalfan Ngassa ambaye amekuwa akifanya vizuri. Ngassa ambaye ni mtoto wa mchezaji wa zamani wa Pamba Jiji na Simba SC, Khalfan Ngassa, pia ni mdogo wa kiungo mshambuliaji wa zamani wa Yanga, Simba na Azam, Mrisho Ngassa anatajwa ni mmoja kati ya wachezaji wanaotazamiwa kufanya makubwa siku za usoni. Mambo Uwanjani Blog itawaletea Makala maalum ya kiungo huyo hatari ambaye ndoto zake ni kufuata nyayo za kaka yake Mrisho Ngassa. Beno Ngassa

HISTORIA YA TIMU YA MASHUJAA YA KIGOMA, KUMBE NI SHEA YA JESHI NA WANANCHI

Timu inaitwa Mashujaa Lake Tanganyika FC ( Mashujaa FC ) ilianza rasmi kampeni yake ya kupanda Ligi Kuu tarehe 29/9/2018 na imepanda Ligi Kuu 25/06/2023 miaka mitano ya kupambana kwenye Ligi Daraja la kwanza Championship. Timu hii inaendeshwa kwa ushirikiano wa pande mbili kati ya Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) na Halmashauri ya Manispaa ya Kigoma Ujiji kwa niaba ya Wananchi wa Kigoma. Muelewe hapa maana wengi wanasema ni timu ya Jeshi asilimia 100% Nembo ya timu ni Sokwe Dume, Shujaa wa Hifadhi za Gombe na Mahale zilizopo mkoani Kigoma. Rangi ya kwanza ya jezi ya timu (first kit) ni hiyo hapo chini na kwenye nembo ya timu ni rangi za tunda la michikichi (mawese ). Hii kama njano ni mawese yaliyoganda na huo wekundu ni mawese ya moto. Ukishika tunda la Mse juu utaona wekundu na ukikata katikati utaona njano. Nyeupe ni ‘nazi’ ya Mse hizi ni alama za utajiri wa Kigoma Jezi nyingine ni blue inayowakilisha Ziwa Tanganyika na Jezi nyingine ni Nyeupe