Ruka hadi kwenye maudhui makuu

CCM NAKO KWAFUKA MOSHI, NAPE APIGWA KOMBORA.

Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Dk Shukuru Kawambwa amejibu madai yaliyotolewa hivi karibuni na Katibu wa Itikadi na Uenezi wa CCM, Nape Nnauye kwamba ni mmoja wa mawaziri walioshindwa kazi, hivyo kustahili kung’olewa.

Katika madai yake, Nape alisema Dk Kawambwa ameshindwa kusimamia vyema madai ya walimu na kwamba akiwa Waziri wa Miundombinu, aliingia mkataba na Kampuni ya ujenzi ya Progressive iliyopewa zabuni ya kujenga Barabara ya Namtumbo hadi Tunduru wakati mkandarasi huyo hana uwezo wa kuijenga.

Nape alikaririwa akisema kwamba umefika wakati kwa waziri huyo na wenzake wa Fedha, Dk William Mgimwa; Kilimo, Chakula na Ushirika, Christopher Chiza; na Naibu wake, Adam Malima kuhojiwa na Kamati Kuu (CC) ya chama hicho.

Akijibu madai hayo Mjini Bagamoyo jana, Dk Kawambwa alisema anasubiri kwa hamu kuitwa CC kueleza tuhuma zinazomkabili huku akijigamba kuwa yeye ni mti wenye matunda ndiyo maana unapigwa mawe.


Alisema hayo alipokuwa akikabidhi vifaa vya michezo kwa timu 16 zitakazoshiriki michuano ya Kombe la Kawambwa inayofanyika katika Jimbo la Bagamoyo ambalo yeye ni mbunge wake.

“Kuna maneno yanayoendelea hivi sasa eti na mimi mbunge wenu natajwa kuwa fisadi kwa mkataba wa ukandarasi wa barabara, siyo kweli. Wakati mkataba ule unasainiwa mimi nilishatoka kwenye Wizara ya Miundombinu, sihusiki kabisa na mkataba ule,” alisema na kuongeza:

“Mwaka 2010 mimi ndiye niliyeshawishi Ubalozi wa Japan ukatoa fedha kwa ajili ya mradi ule wa Barabara ya Namtumbo - Tunduru lakini mkataba ukasainiwa Desemba 24, 2012 kati ya Wizara na Kampuni ya Progressive.

“Walipovurunda Wizara ikawatimua, mimi sikuhusika hata kidogo kwani wakati wanasaini mkataba ule mimi nilishahamishiwa wizara nyingine.”

“Mimi nipo baridi, nasubiri kwa hamu kubwa kuitwa kwenye Kamati Kuu, mimi si mtu wa kupiga kelele na tuhuma zote dhidi yangu ninaamini si za kweli... wakati mwingine maadui wanatafuta njia za kunichonganisha na chama changu.”

“Wanasema kila wizara ninayopelekwa ninavurunda, nasema, mimi ni mti wenye matunda. Mti wowote ambao unazaa vizuri lazima utapigwa mawe, nasubiri siku hiyo ya kuitwa CC ambako pumba na mchele vitajulikana.”

Akizungumzia ujenzi wa barabara hiyo, Waziri Kawambwa alisema anamshukuru  Waziri wa Ujenzi, Dk John Magufuli aliyemfukuza mkandarasi huyo Progressive kwa kushindwa kazi. Hata hivyo, katika madai yake, Nape alisema kumfukuza mkandarasi huyo pekee hakutoshi, bali aliyehusika kumpa mkataba naye anapaswa kuchukuliwa hatua kwani uchunguzi unaonyesha kuwa alishashindwa kazi wakati anapewa mkataba.

Hata hivyo, Katibu Mkuu Kiongozi, Balozi Ombeni Sefue alikaririwa na Gazeti la The Citizen akisema kuwa Chama Cha Mapinduzi hakina mamlaka ya kuingilia utendaji wa Serikali kwani kinatakiwa kuishia katika ngazi za watendaji wa chama.

Machapisho maarufu kutoka blogu hii

FIFA yatoa orodha ya vilabu bora duniani, Simba na Yanga zachuana vikali

SHIRIKISHO la Soka Afrika (CAF) limetoa orodha ya viwango vya ubora wa klabu barani, Simba ikiendelea kuwa juu ya klabu nyingine za Tanzania, nafasi ya tano. Orodha hiyo imetoka leo kuelekea droo ya hatua za awali za michuano ya klabu Afrika ambayo kwa mara ya kwanza kihistoria itafanyika nchini katika studio za Azam Tv, Tabata Jijini Dar es Salaam. Yanga ambayo kama Simba itashiriki Ligi ya Mabingwa — yenyewe inashika nafasi ya 12, wakati timu nyingine katika orodha hiyo ni Namungo FC wanaoshika nafasi ya mwisho, ya 75 kwa pamoja na Salitas FC ya Burkina Faso, Ahli Benghazi ya Libya na NAPSA Stars ya Zambia. Kwa msimu ujao mbali na Simba na Yanga kushiriki Ligi ya Mabingwa, Azam FC na Singida Black Stars zitashiriki michuano ya Kombe la Shirikisho Afrika.

Beno Ngassa mdogo wa Mrisho Ngassa anayekipiga Tanzania Prisons

Miongoni mwa viungo wa pembeni wanaofanya vizuri ni Benodict Khalfan Ngassa ambaye amekuwa akifanya vizuri. Ngassa ambaye ni mtoto wa mchezaji wa zamani wa Pamba Jiji na Simba SC, Khalfan Ngassa, pia ni mdogo wa kiungo mshambuliaji wa zamani wa Yanga, Simba na Azam, Mrisho Ngassa anatajwa ni mmoja kati ya wachezaji wanaotazamiwa kufanya makubwa siku za usoni. Mambo Uwanjani Blog itawaletea Makala maalum ya kiungo huyo hatari ambaye ndoto zake ni kufuata nyayo za kaka yake Mrisho Ngassa. Beno Ngassa

HISTORIA YA TIMU YA MASHUJAA YA KIGOMA, KUMBE NI SHEA YA JESHI NA WANANCHI

Timu inaitwa Mashujaa Lake Tanganyika FC ( Mashujaa FC ) ilianza rasmi kampeni yake ya kupanda Ligi Kuu tarehe 29/9/2018 na imepanda Ligi Kuu 25/06/2023 miaka mitano ya kupambana kwenye Ligi Daraja la kwanza Championship. Timu hii inaendeshwa kwa ushirikiano wa pande mbili kati ya Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) na Halmashauri ya Manispaa ya Kigoma Ujiji kwa niaba ya Wananchi wa Kigoma. Muelewe hapa maana wengi wanasema ni timu ya Jeshi asilimia 100% Nembo ya timu ni Sokwe Dume, Shujaa wa Hifadhi za Gombe na Mahale zilizopo mkoani Kigoma. Rangi ya kwanza ya jezi ya timu (first kit) ni hiyo hapo chini na kwenye nembo ya timu ni rangi za tunda la michikichi (mawese ). Hii kama njano ni mawese yaliyoganda na huo wekundu ni mawese ya moto. Ukishika tunda la Mse juu utaona wekundu na ukikata katikati utaona njano. Nyeupe ni ‘nazi’ ya Mse hizi ni alama za utajiri wa Kigoma Jezi nyingine ni blue inayowakilisha Ziwa Tanganyika na Jezi nyingine ni Nyeupe