Rais wa Shirikisho la Soka Barani Afrika (CAF), Patrice Motsepe, ametangaza rasmi kuanzishwa kwa mashindano mapya ya kimataifa yatakayojulikana kama African Nations League, yenye lengo la kuongeza ushindani na mapato katika soka la Afrika.
Mashindano hayo mapya yanachukua nafasi ya michuano ya mataifa ya Afrika kwa wachezaji wa ligi za ndani (CHAN), huku yakibuniwa kwa mfumo mpya utakaoleta ushindani mkubwa zaidi na kushirikisha wachezaji wa viwango vya juu wanaocheza ndani na nje ya bara la Afrika.
Kwa mujibu wa Motsepe, mashindano hayo yatakuwa na mifumo miwili tofauti ambapo wa kwanza African Nations League Continental, utaendeshwa kwa mfumo wa kanda ambapo timu bora kutoka kila ukanda zitashindana na hatimaye kupata washindi watakaoingia hatua ya fainali itakayofanyika katika nchi mwenyeji.
Pili, African Nations League Pan-African, utakuwa na muundo unaofanana na AFCON, ukizikutanisha timu bora zaidi barani Afrika pamoja na wachezaji nyota wanaocheza katika ligi kubwa duniani.
Motsepe amesema lengo la mashindano hayo ni kuongeza ushindani, kukuza vipaji vya wachezaji wa Afrika, pamoja na kuvutia uwekezaji mkubwa zaidi katika soka la bara hilo.
Hata hivyo, ameweka wazi kuwa CAF inaendelea na mazungumzo na FIFA pamoja na wadau wengine ili kuhakikisha ratiba ya soka duniani inaruhusu mashindano hayo kufanyika bila kuathiri ligi za ndani ambazo tayari zina msongamano wa mechi.
Mashindano hayo mapya yanatarajiwa kuleta sura mpya katika soka la Afrika na kuongeza hadhi ya mashindano ya kimataifa ya bara hilo.

