MALINZI AWASUTA MAREFA WA TANZANIA, ADAI WAMESHAMIRI RUSHWA

RAIS wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), Jamal Malinzi amesema kwamba sekta ya marefa nchini inatia aibu kwa sababu ipo chini mno na amewataka viongozi wa sekta hiyo kuhakikisha wanaiinua juu.

Akizungumza wakati wa kufunga semina ya marefa wa Shirikisho la Soka la Kimataifa (FIFA) kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam, Malinzi amesema kwamba ipo haja ya jitihada kubwa kufanyika kuinua sekta hiyo.


Malinzi amesema baadhi ya nchi jirani ikiwemo Kenya zilikuwa na marefa katika Kombe la Dunia mwaka huu nchini Brazil, lakini Tanzania haikuwa na refa hata mmoja.Amesema hata kwenye michuano mingine ya barani, kama Kombe la Mataifa ya Afrika (AFCON) bado ushiriki wa marefa wa Tanzania ni duni.

Malinzi ameshauri vyuo vya elimu ya juu nchini navyo visaidie kutoa mafunzo ya urefa, akitolea mfano Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM) ambao wana somo la Elimu ya Viungo inayohusu mwili wa mwanamichezo (PE).

“Mfano pale UD (Chuo Kikuu Dar es Salaam) wana somo la PE, kama wataamua kutoa mafunzo ya urefa sisi (TFF) tutakuwa tayari kuwapa ushirikiano ili kuhakikisha tunainua viwango vya marefa nchini,”amesema Malinzi.

Malinzi amesema kwamba amesikitishwa na mkoa wa Ruvuma alipoutembela hivi karibuni na kukuta una marefa wanane tu, wakati ni mkubwa na una wilaya nyingi.
 “Nilishangaa sana, mkoa mkubwa kama ule una marefa wanane tu, sasa huyo bingwa wa mkoa anapatikana vipi, kwa kweli hali ni mbaya sana,”amesema.

Malinzi amesema baada ya hali hiyo, ameagiza TFF ifanye tathmini ya kujua kila mkoa una marefa wangapi ili kujua sehemu ambazo wana mapungufu waelekeze nguvu ya kuinua marefa.

Amesema ipo haja ya waamuzi wastaafu, wakongwe na viongozi wa marefa kushirikiana kuinua marefa chipukizi katika viwango vizuri ili taifa liwe na marefa wa kutosha siku za usoni.

Pamoja na hayo, Malinzi amewaasa marefa kujiepusha na rushwa- kwani soka ya Tanzania kwa sasa inanyemelewa na maharamia wa kimataifa wa kupanga matokeo ili kujinufaisha katika mchezo wa kamari.

“Nina ushahidi wa kutosha mechi za Tanzania sasa zinachezewa kamari nje ya nchi, sasa hii ni hatari sana kwa soka yetu, naomba sana mjiepushe na upangaji wa matokeo,”amesema.

Malinzi amesema TFF inawafanyia uchunguzi marefa wawili kwa tuhuma za kupanga matokeo ambao kwa sasa wamesimamishwa ili kupisha uchunguzi huo, na ikibainika ni kweli watachukuliwa hatua kali za kisheria.

“Nchi za wenzetu ukigundulika ulihusika na upangaji wa matokeo, unapelekwa mahakamani sheria inafuata mkondo wake, sasa na sisi tutafanya nini, kwa hiyo naomba sana tujiepushe na upangaji wa matokeo,”Malinzi aliwaambia marefa huyo.

Semina hiyo iliendeshwa na mkufunzi wa Shirikisho la Soka la Kimataifa (FIFA), Carlos Henriuques kutoka Afrika Kusini ambaye ni Ofisa Maendeleo ya Marefa wa shirikisho hilo.

Machapisho maarufu kutoka blogu hii

HISTORIA YA TIMU YA MASHUJAA YA KIGOMA, KUMBE NI SHEA YA JESHI NA WANANCHI

MAKALA: SIMBA NI TIMU YA KWANZA TANZANIA KUINGIA NUSU FAINALI AFRIKA

STAA WETU: JEREMIA JUMA MTOTO WA JUMA MGUNDA ALIYEIKACHA SIMBA NA KUENDELEA NA UASKARI