Na Prince Hoza Matua
NAMSHANGAA sana aliyekuwa Rais wa klabu ya Yanga SC, Tarimba Abbas Tarimba ambaye pia ni mbunge wa Jimbo la Kinondonj kupitia Chama Cha Mapinduzi, CCM.
Tarimba amezungumza mengi kuhusu klabu yake ya Yanga SC ambapo pia yeye ni mfadhili kupitia kampuni yake ya Sportpesa, kigogo huyo wa Yanga na Tanzania kwa ujumla alikosoa sajili zinazofanywa na klabu hiyo kwa siku za karibuni akidai kwamba si nzuri.
Kwa kifupi Tarimba amechukizwa na matokeo ya timu hiyo iliyoyapata Jumapili iliyopita ilipocheza na hasimu wake Simba SC katika uwanja wa New Amaan Stadium, mjini Zanzibar.
Katika mchezo huo Yanga ililazimishwa sare tasa na Simba ya 0-0, sio siri matokeo hayo ya sare yaliwahudhi mashabiki wengi wa timu hiyo yenye maskani yake mitaa ya Twiga na Jangwani, Kariakoo jijini Dar es Salaam.
Tarimba amepeleka malalamiko yake moja kwa moja kwa Rais wa sasa wa klabu hiyo Injinia Hersi Ally Said ambaye pia amekuwa akihusika moja kwa moja kufanya sajili za wachezaji wapya.
Wanayanga wengi wanamlaumu Injinia Hersi wakidai ameboronga katika sajili za dirisha kubwa na hata dogo la Januari mwaka huu, lakini wengine wanapeleka malalamiko yao kwa kocha mkuu wa timu hiyo, Mreno, Pedro Goncalves.
Kocha anatupiwa macho huku wengine wakitaka avunjiwe mkataba kutokana na timu kutocheza vema, Yanga imetolewa katika hatua ya makundi Ligi ya mabingwa Afrika huku pia ikilazimishwa sare na hasimu wake Simba ambaye kwa kipindi cha miaka mitatu imekuwa ikiwafunga mfululizo.
Yanga imewafunga Simba mara sita mfululizo hivyo kitendo cha kulazimika sare haikubaliki, Mheshimiwa Tarimba amewaamsha Wanayanga kwamba Injinia Hersi amekosea kufanya usajili na pia kocha Pedro hafai.
Kwa upande wa Injinia Hersi namtetea jamani, mpaka sasa sajili zake alizofanya asilimia 79 ikafanikiwa, kwani timu yake inafanya vizuri kwenye mashindano ya ndani na pia ya kimataifa ingawa haikavuka kwenda hatua nyingine.
Katika mashindano ya ndani, timu ya Injinia imeshinda mataji yote lawama Yanini! lakini pia kimataifa Injinia Hersi amekuwa akisikika wazi wazi kwamba malengo ya Yanga ni kufika hatua ya makundi Ligi ya mabingwa na mara zote timu yake imekuwa ikifanya hivyo.
Tarimba anapaswa kumuomba radhi Injinia Hersi na Yanga kwa ujumla, kwani kauli yake inaweza kuchangia mgogoro-, kuhusu Pedro, asilaumiwe kwani mpinzaji wake Simba SC alikuwa kwenye ubora wa hali ya juu na alistahili kuondoka na ushindi tena ni zaidi ya goli moja.
Kwa kifupi katika mchezo huo wa watani wa jadi, mashabiki wa Yanga hawapaswi kumlaumu kocha wao na zaidi wanatakiwa kumsifu kwa kutengeneza vema safu ya ulinzi na kuhakikisha Simba hawapati hata bao.
Simba chini ya kocha wao Steve Barker raia wa Afrika Kusini wamecheza vizuri sana kuwazidi Yanga kwenye eneo la katikati ya uwanja na kufanya mashambulizi mengi langoni kwa Yanga, shukrani kubwa kwa Yanga inaendwa na mabeki wake wakisaidiana na Djigui Diarra ambaye alikuwa golini.
Diarra alicheza saves nyingi na kuwazuia Simba wasimfunge kihalali, kwa upande wa Pedro katika mchezo huo alianza na kikosi cha kuzuia kwani viungo wake wote aliowaanzisha ni wazuiaji.
Kukosekana kwa Pacome Zouzoua na mshambuliaji Clement Mzize kimesababisha kocha huyo aamue kujilinda zaidi kuliko kufunguka na huenda ingemuathiri zaidi kupata matokeo mazuri.
Pedro aliona hata kama Yanga ingefungwa asingepoteza kitu kwani nafasi ya uongozi kwenye Ligi ingeendelea kuwa yake, lakini alihakikisha anapanga viungo wakabaji Ili angalau kupata sare na jambo ambalo amefanikiwa.
Mpango wake timu kuongoza ligi amefanikiwa na pia timu yake isifungwe dhidi ya Simba, kumlaumu Pedro ni sawa na kumuhukumu bila hatia kwani mpaka sasa Yanga ya Pedro inaongoza ligi kwa tofauti ya pointi tano kabla ya mchezo wake na Singida Black Stars.
ALAMSIKI
