Inaandikwa na Fikiri Salum
HISTORIA ya Afrika ni historia ya bara hilo lililo asili ya binadamu wote, kwa ujumla, historia ni kumbukumbu ya maisha ya mwanadamu duniani hasa Ile tarehe iliyosajiliwa na kuhifadhiwa katika vitabu, maandishi mbalimbali, na simulizi au hekaya za mapokeo.
Ingawa historia iliyobebwa katika simulizi za hekaya huchukuliwa na baadhi kuwa haina nguvu kwa kukosa ithibati ya maandishi, bado hivi ni vyanzo muhimu vya historia.
Mara nyingi historia iliyoko katika maandishi huwa imehifadhiwa katika simulizi na hekaya kwa muda mrefu kabla ya kuandikwa.
HISTORIA YA AFRIKA
Hapo kale, bara la Afrika lilishuhudia matukio mengi ya harakati za mwanadamu kuliko mabara mengine ya ulimwenguni.
Wataalamu wa athali wamegundua athali za Zamadamu zinarudi nyuma kufikia hadi miaka ya milioni nne, na athali za ustaarabu wa Wamisri wa kale huko Misri na Wafoinike huko Tunis na sehemu nyinginezo za Afrika kaskazini katika karne ya 9 KK.
Harakati za madola makubwa ya Wazungu na Waarabu ziliweza kuonekana kabla ya karne ya 4 BK, na Waarabu walianza kuingia Afrika huko Habasha (Ethiopia) tangu karne ya 7 BK na kutangaza dini ya Uislamu na kueneza katika maeneo mbalimbali ya Afrika pamoja na kuanzisha biashara na ustaarabu na kuimarisha mamlaka zao katika Sudan ya wakati huo tangu karne ya 8 baada ya Kristo.
Himaya- za Ghana, Mali na Songhai zilikuwa zikijulikana kwa utajiri mkubwa na biashara stawi, iliyokuwa ikifanyika wakati huo ya dhahabu na bidhaa nyinginezo.
Mwisho wa karne ya 15 BK, himaya ya Songhai ilikuwa na nguvu kuweza kuita chini ya utawala wake mamlaka ya Mali, sehemu nyingine za kusini mwa Afrika zilikuwa wakati huu hazijulikani sana, na historia yake ilikuwa bado haijadajiliwa.
Baina ya karne ya 1 KK na karne ya 16 BK watu waliokuwa wakizungumza lugha ya Kibantu watokao sehemu za Nigeria na Cameroon ya leo ndio waliokuwa wameenea kwenye sehemu mbalimbali kusini mwa bara la Afrika, wakiwa wameanzisha vijiji, mashamba na mamlaka katika sehemu ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo ya leo.
Maeneo mengine ni Zaluba na Mwememutapa, lakini makundi ya wachungaji wa wanyama walianza kuhamia kusini katika karne za 15 na 16 na kukutana na Wabantu, ndipo walipoanzisha mamlaka zao za Bunyoro, Buganda, Rwanda na Ankole.
UKOLONI
Wazungu walianza kugundua bara la Afrika katika karne ya 15, wakati Wareno walipokuja kwenye fukwe za bara la Afrika kutafuta njia nyepesi na ya amani ya kufikia India, na kuweza kupata nafasi ya kushikilia biashara ya dhahabu na pembe na watumwa ambayo ilikuwa ikiendelea wakati huo katika bara la Afrika.
INAENDELEA
