Mahakama ya Usuluhishi wa Michezo (CAS) imethibitisha kupokea rufaa ya Senegal inayopinga uamuzi wa Bodi ya Rufaa ya CAF kuwapoka ubingwa wa AFCON 2025.
Rufaa hiyo ilisajiliwa rasmi na CAS Machi 25, 2026, ambapo Shirikisho la Soka la Senegal (FSF) inalenga: kufuta uamuzi wa CAF na kutangazwa rasmi kuwa wao ndio mabingwa halali wa AFCON 2025.
CAS imebainisha kuwa jopo la usuluhishi litaundwa kuchunguza kesi na kuweka ratiba ya kesi. Kwa mujibu wa kanuni za sasa, mshitakiwa ana siku ishirini za kuwasilisha hoja zake za kisheria.
Katika uamuzi wa kihistoria, Bodi ya Rufaa ya CAF iliamua kwamba Timu ya Taifa ya Senegal ilipoteza fainali ya AFCON baada ya wachezaji kadhaa kutoka uwanjani hadi kwenye chumba chao cha kubadilishia nguo wakipinga uamuzi wa mwamuzi.
Uamuzi huo ulisema Senegal ilikiuka vifungu vya 82 na 84 vya kanuni za AFCON walipotoka uwanjani wakati wa mchezo.
Pia itakumbukwa kuwa takribani mashabiki 18 wamefungwa nchini Morocco baada ya kupatikana na hatia ya kuhusika katika vurugu wakati wa fainali hiyo iliyofanyika nchini Morocco.
