Ruka hadi kwenye maudhui makuu

STARS YALAZIMISHWA SARE NYUMBANI

TANZANIA, Taifa Stars imeanza vibaya hatua ya mwisho ya mchujo kuwania kupangwa kwenye makundi ya kuwania tiketi ya kucheza Fainali za Mataifa ya Afrika mwakani nchini Morocco, baada ya kulazimishwa sare ya 2-2 na Msumbiji.

Katika mchezo huo, uliofanyika Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam jana, mabao ya Stars inayofundishwa na Mholanzi Mart Nooij yalifungwa na kiungo wa Azam FC, Khamis Mcha ‘Vialli’ aliyeingia kipindi cha pili kuchukua nafasi ya Mrisho Ngassa.


Dakika 45 za kwanza zilimalizika bila bao na kipindi cha pili, Msumbiji walikuwa wa kwanza kupata bao dakika ya 47 kwa penalti iliyokwamishwa nyavuni na Elias Pelembe baada ya Kevin Yondan kucheza rafu kwenye eneo la hatari. Mcha aliisawazishia Stars bao hilo dakika ya 65 akimalizia kazi nzuri ya Thomas Ulimwengu.

Mcha tena akaifungia Stars bao lililoelekea kuwa la ushindi dakika ya 71 kwa penalti, baada ya mabeki wa Mambas kumchezea rafu Mbwana Samatta kwenye eneo la hatari.

Stars iliongeza mashambulizi langoni mwa Msumbiji na kukosa mabao kadhaa ya wazi. Msumbiji walizinduka na kufanya shambulizi zuri lililowapatia bao la kusawazisha dakika ya 87 kupitia kwa Isaac Carvalho aliyetokea benchi pia.

Kwa matokeo, hayo Stars sasa itajitaji ushindi wa ugenini ili kusonga mbele, au sare ya kuanzia mabao 3-3, wakati wenyeji wanaweza kunufaika na sare ya 1-1 au 0-0. Ikiwa 2-2 tena, mshindi ataamuliwa kwa mikwaju ya penalti.

Stars iliyofika hatua hii baada ya kuitoa Zimbabwe kwa jumla ya mabao 3-2 ikishinda 1-0 nyumbani na sare ya 2-2 Harare, ikifanikiwa kuitoa Msumbiji itapangwa katika Kundi C ambalo lina timu za Zambia, Cerpe Verde na Niger zilizofuzu moja kwa moja hatua hiyo, kuwania tiketi ya Morocco mwakani.

Stars imekuwa ikinyanyaswa na Msumbiji miaka ya karibuni na mara mbili imewahi kutolewa na Mambas katika hatua za awali za AFCON. Kuwania Fainali za Ghana mwaka 2008, Stars ikiwa chini ya kocha Mbrazil, Marcio Maximo ilifungwa 1-0 Dar es Salaam katika mchezo wa mwisho wa kundi.

Kuwania Fainali za mwaka jana Afrika Kusini, Stars ikiwa chini ya kocha Mdenmark, Kim Poulsen, ilitolewa kwa penalti 5-4 na Msumbiji baada ya sare ya jumla ya 2-2.

Kikosi cha Tanzania kilikuwa; Deogratius Munishi ‘Dida’, Shomary Kapombe, Oscar Joshua, Kevin Yondan, Nadir Haroub ‘Cannavaro’, Mwinyi Kazimoto, Thomas Ulimwengu, Erasto Nyoni, John Bocco/Haroun Chanongo dk78, Mbwana Samatta/Simon Msuva dk83 na Mrisho Ngassa/Khamis Mcha dk57.

Msumbiji; Dario Khan, Momed Hagi, Zainadine Junior, Saddan Guambe, Francisco Mioche, Eduardo Jumisse/Isaac de Carvalho dk85, Elias Pelembe, Josemar Machaisse, Helder Pelembe, Almiro Lobo na Richard Campos.

Machapisho maarufu kutoka blogu hii

FIFA yatoa orodha ya vilabu bora duniani, Simba na Yanga zachuana vikali

SHIRIKISHO la Soka Afrika (CAF) limetoa orodha ya viwango vya ubora wa klabu barani, Simba ikiendelea kuwa juu ya klabu nyingine za Tanzania, nafasi ya tano. Orodha hiyo imetoka leo kuelekea droo ya hatua za awali za michuano ya klabu Afrika ambayo kwa mara ya kwanza kihistoria itafanyika nchini katika studio za Azam Tv, Tabata Jijini Dar es Salaam. Yanga ambayo kama Simba itashiriki Ligi ya Mabingwa — yenyewe inashika nafasi ya 12, wakati timu nyingine katika orodha hiyo ni Namungo FC wanaoshika nafasi ya mwisho, ya 75 kwa pamoja na Salitas FC ya Burkina Faso, Ahli Benghazi ya Libya na NAPSA Stars ya Zambia. Kwa msimu ujao mbali na Simba na Yanga kushiriki Ligi ya Mabingwa, Azam FC na Singida Black Stars zitashiriki michuano ya Kombe la Shirikisho Afrika.

Beno Ngassa mdogo wa Mrisho Ngassa anayekipiga Tanzania Prisons

Miongoni mwa viungo wa pembeni wanaofanya vizuri ni Benodict Khalfan Ngassa ambaye amekuwa akifanya vizuri. Ngassa ambaye ni mtoto wa mchezaji wa zamani wa Pamba Jiji na Simba SC, Khalfan Ngassa, pia ni mdogo wa kiungo mshambuliaji wa zamani wa Yanga, Simba na Azam, Mrisho Ngassa anatajwa ni mmoja kati ya wachezaji wanaotazamiwa kufanya makubwa siku za usoni. Mambo Uwanjani Blog itawaletea Makala maalum ya kiungo huyo hatari ambaye ndoto zake ni kufuata nyayo za kaka yake Mrisho Ngassa. Beno Ngassa

HISTORIA YA TIMU YA MASHUJAA YA KIGOMA, KUMBE NI SHEA YA JESHI NA WANANCHI

Timu inaitwa Mashujaa Lake Tanganyika FC ( Mashujaa FC ) ilianza rasmi kampeni yake ya kupanda Ligi Kuu tarehe 29/9/2018 na imepanda Ligi Kuu 25/06/2023 miaka mitano ya kupambana kwenye Ligi Daraja la kwanza Championship. Timu hii inaendeshwa kwa ushirikiano wa pande mbili kati ya Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) na Halmashauri ya Manispaa ya Kigoma Ujiji kwa niaba ya Wananchi wa Kigoma. Muelewe hapa maana wengi wanasema ni timu ya Jeshi asilimia 100% Nembo ya timu ni Sokwe Dume, Shujaa wa Hifadhi za Gombe na Mahale zilizopo mkoani Kigoma. Rangi ya kwanza ya jezi ya timu (first kit) ni hiyo hapo chini na kwenye nembo ya timu ni rangi za tunda la michikichi (mawese ). Hii kama njano ni mawese yaliyoganda na huo wekundu ni mawese ya moto. Ukishika tunda la Mse juu utaona wekundu na ukikata katikati utaona njano. Nyeupe ni ‘nazi’ ya Mse hizi ni alama za utajiri wa Kigoma Jezi nyingine ni blue inayowakilisha Ziwa Tanganyika na Jezi nyingine ni Nyeupe