Ripoti mbalimbali kutoka vyanzo vya kuaminika nchini Saudi Arabia zinaeleza kuwa nyota wa kimataifa Cristiano Ronaldo, amesitisha rasmi mgomo wake na yuko tayari kurejea uwanjani kuitumikia klabu ya Al Nassr, baada ya wafanyakazi wote wa klabu hiyo kulipwa mishahara na posho zao walizokuwa wanadai.
Hatua hiyo inakuja baada ya mvutano uliodumu kwa muda kati ya Ronaldo na Tume ya Uwekezaji ya Saudi Arabia, inayofahamika kama Saudi Public Investment Fund (PIF).
Inadaiwa kuwa nahodha huyo wa timu ya taifa ya Ureno alikuwa na malalamiko makubwa kuhusu kile alichodai kuwa ni upendeleo unaotolewa kwa baadhi ya klabu, hususan katika masuala ya usajili wa wachezaji na uwekezaji, jambo ambalo aliona linaathiri ushindani wa haki ndani ya ligi.
Mbali na kulalamikia mwenendo wa usajili ambao haukuwa na tija kwa Al Nassr, Ronaldo pia alichukua msimamo mkali wa kugoma kushiriki mazoezini na mechi ili kushinikiza haki za wafanyakazi wa klabu hiyo, hasa wale wa ngazi za chini, ambao kwa muda walikuwa hawajalipwa stahiki zao.
Kwa mujibu wa taarifa hizo, Ronaldo alisisitiza kuwa heshima na ustawi wa wafanyakazi ni msingi muhimu wa mafanikio ya klabu yoyote.
Baada ya madai hayo kushughulikiwa na malipo kufanyika kwa wafanyakazi wote, Ronaldo ameridhia kurejea kikosini na kuendelea na majukumu yake ya kuiongoza Al Nassr uwanjani.
Kurejea kwake kunatarajiwa kuipa nguvu mpya timu hiyo katika michezo ijayo, huku mashabiki wakitarajia kuona nahodha wao akirejea katika kiwango chake cha juu na kuisaidia klabu kupigania malengo yake ndani na nje ya Saudi Arabia.
