Les Aigles du Congo mabingwa wapya DRC

TIMU ya FC Les Aigles du Congo (Eagles of Congo) ya Kinshasa imefanikiwa kutwaa ubingwa wa Ligi Kuu ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC) ijulikanayo kama Linafoot kwa mara ya kwanza katika historia yake baada ya kutoa sare ya kufungana bao 1-1 na TP Mazembe Ijumaa ya jana (Juni 27, 2025) Uwanja wa Kamalondo, Lubumbashi.

Beki Heltone Kayembe alianza kuifungia Aigle du Congo ‘Des Samourais’, (The Samurai) dakika ya 35 akimtungua kipa Baggio Siadi Ngusia, kabla ya Patrick Mwaungulu kuisawazishia TP Mazembe dakika ya 47 akimtungua kipa Nathan Dibu kufuatia kazi nzuri ya Patient Mwamba.

Kwa matokeo hayo, Aigles du Congo inayofundishwa na Kocha wa zamani wa Tabora United, Anicet Kiazayidi inamaliza na pointi 35 kileleni mwa Linafoot ikifuatiwa na FC Saint Eloi Lupopo ya Lubumbashi pia yenye pointi 33 baada ya mechi 16 kwenye ligi ya timu 12 na zote zinafuzu Ligi ya Mabingwa Afrika msimu ujao.
Timu ya AS Maniema iliyomaliza nafasi ya tatu kwa pointi zake 32 inakwenda Kombe la Shirikisho Afrika katika msimu ambao umekuja na mageuzi makubwa katika Linafoot, kwani hata kigogo mmoja wa kihistoria, iwe Mazembe, AS Vita Club wala DC Motemba Pembe aliyepenya nafasi tatu za juu.

TP Mazembe ya Kocha Msenegal, Lamine N'Diaye, waliokuwa mabingwa watetezi, wamemaliza nafasi ya nne kwa pointi zao 30 nyuma ya Motema Pembe iliyovuna pointi 31.

FC Les Aigles du Congo ni klabu iliyoanzishwa na Mfanyabiashara na Mwanasiasa, Vidiye Tshipanda Tshimanga mwaka 2023 yenye maskani yake Jjini Kinshasa, ambaye aliinunua klabu ya Jeunesse Sportive de Kinshasa maarufu kama JSK na kuibadili jina.

Kisiasa Vidiye Tshipanda Tshimanga (48) ni Mshauri wa Rais wa DRC, Felix Tshisekedi Tshilombo juu ya masuala
maalum a ya kimkakati.