Ruka hadi kwenye maudhui makuu

MALINZI KUMLIPA POULSEN ILI AONDOKE

Rais  wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), Jamal Malinzi, amesema atalipa nusu ya gharama zilizotokana na shirikisho hilo kuvunja mkataba wa aliyekuwa Kocha Mkuu wa timu ya Taifa (Taifa Stars), Kim Poulsen.

Hata hivyo, Malinzi na Kim hawakutaka kuweka wazi hatua walizofikia baada ya kuamua kuvunja mkataba zaidi ya kueleza kuwa walifikia makubaliano ya pamoja.

Akizungumza jana jijini Dar es Salaam, Malinzi alisema sehemu nyingine ya gharama ya fedha zilizobakia zitalipwa na shirikisho hilo na waliamua kusitisha mkataba wa Kim ili wasake kocha mpya ambaye moja ya sifa zake ni kuwahi kuipeleka timu mojawapo ya Afrika kwenye fainali za Kombe la Mataifa ya Afrika, AFCON.


Malinzi alisema serikali haihusiki na maamuzi hayo yaliyofikiwa na TFF ila ilijulishwa hatua zote za mchakato huo na kuelezwa tayari wameshaanza kusaka kocha atakayerithi mikoba ya Mdenmark huyo.

"Tulichokubaliana ni siri na kitabaki kuwa siri, TFF tutabeba, wapo wadau waliojitokeza kutulipia nusu kwa sababu waliahidi kuwa huu ni wakati wa mabadiliko," alisema Malinzi na baadaye kubadili kauli ya wadau na kujitaja yeye kuwa ndiye atakayelipa gharama hizo.

Aliongeza kwamba tayari TFF imeshabaki na majina matatu (hakuyataja) ya makocha ambao mmoja wao ataajiriwa akisema wawili wanatoka Uholanzi na mwingine ni raia wa Ujerumani.

"Jukumu lake kubwa litakuwa ni kuendeleza soka la vijana na atachagua msaidizi wake," aliongeza.

Alimtaja Kaimu Mkurugenzi wa Ufundi, Salum Madadi, ambaye ana leseni Daraja A kuwa ndiye atakaimu nafasi ya Poulsen na ataiongoza Taifa Stars katika mechi moja itakayochezwa Machi 5 jijini Windhoek, Namibia.

POULSEN ANENA

Naye, Poulsen  aliwashukuru wachezaji, benchi la ufundi, wadhamini (Kampuni ya Bia Tanzania- TBL), mashabiki na wadau wote wa soka nchini kwa kumpa ushirikiano katika kipindi chote alichokuwa hapa nchini tangu Mei, 2012.

"Kunapokuja uongozi mpya lazima vitu kama hivi hutokea, uongozi mpya wa TFF umefanya mabadiliko mengi katika uongozi wake, hivyo hata mimi sishangai kuona nafukuzwa ingawa nimesaidia kwa kiasi kikubwa kuleta mafanikio ya soka la Tanzania," alisema Poulsen.

Raia huyo wa Denmark alisema alikuta Tanzania ikiwa nafasi za chini katika viwango vya Fifa lakini sasa iko nafasi iko vizuri na ameiwezesha Taifa Stars kuzifunga timu ngumu za Zambia, Cameroon na Morocco.

"Kuna baadhi ya mechi tulifungwa kwa sababu ya mazingira yetu, mnakwenda kucheza  na timu ngumu huku wachezaji wenu hawana lishe ya uhakika, tuliangushwa na lishe katika mechi ya mwisho ya kuwania kufuzu Kombe la Dunia," alisema Poulsen.

Alisema hata hivyo anaheshimu maamuzi ya viongozi wapya wa TFF ambao wanaamini wako sahihi.

Poulsen aliishukuru ajira aliyokuwa nayo Stars kwamba imemwezesha kupata kazi ya ukufunzi wa makocha wa FIFA na akaongeza atakuwapo nchini hadi atakapolipwa fedha zake.

Mwenyekiti wa Kamati ya Ufundi, Alfred Kidau, alisema idara yake iko wazi na mabadiliko yaliyofanywa kwenye benchi la ufundi yalikuwa ni ya nia njema.

Machapisho maarufu kutoka blogu hii

FIFA yatoa orodha ya vilabu bora duniani, Simba na Yanga zachuana vikali

SHIRIKISHO la Soka Afrika (CAF) limetoa orodha ya viwango vya ubora wa klabu barani, Simba ikiendelea kuwa juu ya klabu nyingine za Tanzania, nafasi ya tano. Orodha hiyo imetoka leo kuelekea droo ya hatua za awali za michuano ya klabu Afrika ambayo kwa mara ya kwanza kihistoria itafanyika nchini katika studio za Azam Tv, Tabata Jijini Dar es Salaam. Yanga ambayo kama Simba itashiriki Ligi ya Mabingwa — yenyewe inashika nafasi ya 12, wakati timu nyingine katika orodha hiyo ni Namungo FC wanaoshika nafasi ya mwisho, ya 75 kwa pamoja na Salitas FC ya Burkina Faso, Ahli Benghazi ya Libya na NAPSA Stars ya Zambia. Kwa msimu ujao mbali na Simba na Yanga kushiriki Ligi ya Mabingwa, Azam FC na Singida Black Stars zitashiriki michuano ya Kombe la Shirikisho Afrika.

HISTORIA YA TIMU YA MASHUJAA YA KIGOMA, KUMBE NI SHEA YA JESHI NA WANANCHI

Timu inaitwa Mashujaa Lake Tanganyika FC ( Mashujaa FC ) ilianza rasmi kampeni yake ya kupanda Ligi Kuu tarehe 29/9/2018 na imepanda Ligi Kuu 25/06/2023 miaka mitano ya kupambana kwenye Ligi Daraja la kwanza Championship. Timu hii inaendeshwa kwa ushirikiano wa pande mbili kati ya Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) na Halmashauri ya Manispaa ya Kigoma Ujiji kwa niaba ya Wananchi wa Kigoma. Muelewe hapa maana wengi wanasema ni timu ya Jeshi asilimia 100% Nembo ya timu ni Sokwe Dume, Shujaa wa Hifadhi za Gombe na Mahale zilizopo mkoani Kigoma. Rangi ya kwanza ya jezi ya timu (first kit) ni hiyo hapo chini na kwenye nembo ya timu ni rangi za tunda la michikichi (mawese ). Hii kama njano ni mawese yaliyoganda na huo wekundu ni mawese ya moto. Ukishika tunda la Mse juu utaona wekundu na ukikata katikati utaona njano. Nyeupe ni ‘nazi’ ya Mse hizi ni alama za utajiri wa Kigoma Jezi nyingine ni blue inayowakilisha Ziwa Tanganyika na Jezi nyingine ni Nyeupe

Beno Ngassa mdogo wa Mrisho Ngassa anayekipiga Tanzania Prisons

Miongoni mwa viungo wa pembeni wanaofanya vizuri ni Benodict Khalfan Ngassa ambaye amekuwa akifanya vizuri. Ngassa ambaye ni mtoto wa mchezaji wa zamani wa Pamba Jiji na Simba SC, Khalfan Ngassa, pia ni mdogo wa kiungo mshambuliaji wa zamani wa Yanga, Simba na Azam, Mrisho Ngassa anatajwa ni mmoja kati ya wachezaji wanaotazamiwa kufanya makubwa siku za usoni. Mambo Uwanjani Blog itawaletea Makala maalum ya kiungo huyo hatari ambaye ndoto zake ni kufuata nyayo za kaka yake Mrisho Ngassa. Beno Ngassa