Ruka hadi kwenye maudhui makuu

TAMBWE AZIDI KUTIKISA LIGI KUU

Mshambuliaji Amisi Tambwe (Pichani) jana alifunga goli lake la saba katika mechi tatu wakati alipoiongoza Simba kushinda 2-0 dhidi ya JKT Ruvu kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam na kujiimarisha kileleni mwa msimamo wa Ligi Kuu ya Tanzania Bara.


Tambwe ambaye amejiunga na Simba katika kipindi kilichoisha cha usajili akitokea kuipa ubingwa wa Kombe la Kagame la Klabu Bingwa Afrika Mashariki na Kati timu ya Vital'O ya kwao Burundi, alifunga goli la kuongoza katika ya dakika 25 kwa penalti.

Simba ilipata penalti hiyo baada ya beki wa kati wa JKT Ruvu, Omar Mtaki kuonekana ameunawa mpira wa krosi iliyopigwa na haruna Chanongo. Refa wa kati hakuona kama kuna madhambi yamefanyika lakini mwamuzi wa pembeni John Kanyenye kuotoa Mbeya aliamua kuwa ni penalti.

Wachezaji wa JKT Ruvu waliilalamikia sana penalti hiyo huku mtunza vifaa wao, Selemani Oga, akiingia uwanjani kumzonga mwamuzi.

Hali hiyo iliendelea hata baada ya mechi hiyo kumalizika pale mchezaji Paul Ndauka alipoingia uwanjani kumzonga mwamuzi huyo ambaye alijaribu kumkwepa kwa kurudirudi nyuma.
Matokeo hayo yalidumu hadi wakati wa mapumziko.

Kipindi cha pili JKT Ruvu walirejea kwa kasi kwa nia ya kusawazisha goli hilo, lakini kushambulia mfululizo kuliwagharimu kwani walijikuta wakifungwa goli la pili kwa shambulizi la kustukiza.

Kiungo Abdulhalim Homoud alikimbia na mpira kutokea katikati ya uwanja kabla ya kupiga krosi iliyomkuta Ramadhan Singano 'Messi' aliyeusukumia mpira wavuni kwa mguu wa kulia, ikiwa ni dakika sita tu baada ya mapumziko. Messi alikuwa ameingia uwanjani katika dakika ya 36 kuchukua nafasi ya Amri Kiemba.

Kwa ushindi huo, Simba imefikisha pointi 14 kileleni baada ya mechi saba.

Katika mechi nyingine, Azam FC iling'ang'aniwa kwa sare ya 1-1 dhidi ya Prisons kwenye Uwanja wa Sokoine mjini Mbeya. Wenyeji Prisons walitangulia kupata goli katika dakika ya 36 lililofungwa na Peter Michael kabla ya Azam kusawazisha kupitia kwa Kipre Tchetche katika dakika ya 49.

Kwenye Uwanja wa Azam Complex, timu inayoburuta mkia ya Ashanti United ilipata pointi yake ya pili tangu irejee kwenye Ligi Kuu msimu huu baada ya kulazimisha sare ya 2-2 dhidi ya Mtibwa Sugar. Ashanti ilipata magoli yake kupitia kwa Paul Maone na Tumba Swedi, wakati ya Mtibwa yalifungwa na Shaaban Kisiga.

Vikosi kwenye Uwanja wa Taifa vilikuwa; Simba: Abbel Dhaira, Haruna Shamte, Adeyoum Seif, Kaze Gilbert, Joseph Owino, Abdulhalim Humoud, Amri Kiemba/ Ramadhani Singano (dk. 36), Said Ndemla, Betram Mombeki/ Miraj Madenge (dk. 73), Amisi Tambwe na Haroun Chanongo/Marcel Kaeza (dk. 57).

JKT Ruvu: Shaaban Dihile, Damas Makwaya, Stanley Nkomola, Omar Mtaki, Jamal Said, Nashon Naftali, Alhaj Zege, Emanuel Swita/ Richard Msenya (dk. 58), Bakari Kondo/ Paul Ndauka (dk.78), Salum Machaku na Emmanuel Pius.

Machapisho maarufu kutoka blogu hii

FIFA yatoa orodha ya vilabu bora duniani, Simba na Yanga zachuana vikali

SHIRIKISHO la Soka Afrika (CAF) limetoa orodha ya viwango vya ubora wa klabu barani, Simba ikiendelea kuwa juu ya klabu nyingine za Tanzania, nafasi ya tano. Orodha hiyo imetoka leo kuelekea droo ya hatua za awali za michuano ya klabu Afrika ambayo kwa mara ya kwanza kihistoria itafanyika nchini katika studio za Azam Tv, Tabata Jijini Dar es Salaam. Yanga ambayo kama Simba itashiriki Ligi ya Mabingwa — yenyewe inashika nafasi ya 12, wakati timu nyingine katika orodha hiyo ni Namungo FC wanaoshika nafasi ya mwisho, ya 75 kwa pamoja na Salitas FC ya Burkina Faso, Ahli Benghazi ya Libya na NAPSA Stars ya Zambia. Kwa msimu ujao mbali na Simba na Yanga kushiriki Ligi ya Mabingwa, Azam FC na Singida Black Stars zitashiriki michuano ya Kombe la Shirikisho Afrika.

HISTORIA YA TIMU YA MASHUJAA YA KIGOMA, KUMBE NI SHEA YA JESHI NA WANANCHI

Timu inaitwa Mashujaa Lake Tanganyika FC ( Mashujaa FC ) ilianza rasmi kampeni yake ya kupanda Ligi Kuu tarehe 29/9/2018 na imepanda Ligi Kuu 25/06/2023 miaka mitano ya kupambana kwenye Ligi Daraja la kwanza Championship. Timu hii inaendeshwa kwa ushirikiano wa pande mbili kati ya Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) na Halmashauri ya Manispaa ya Kigoma Ujiji kwa niaba ya Wananchi wa Kigoma. Muelewe hapa maana wengi wanasema ni timu ya Jeshi asilimia 100% Nembo ya timu ni Sokwe Dume, Shujaa wa Hifadhi za Gombe na Mahale zilizopo mkoani Kigoma. Rangi ya kwanza ya jezi ya timu (first kit) ni hiyo hapo chini na kwenye nembo ya timu ni rangi za tunda la michikichi (mawese ). Hii kama njano ni mawese yaliyoganda na huo wekundu ni mawese ya moto. Ukishika tunda la Mse juu utaona wekundu na ukikata katikati utaona njano. Nyeupe ni ‘nazi’ ya Mse hizi ni alama za utajiri wa Kigoma Jezi nyingine ni blue inayowakilisha Ziwa Tanganyika na Jezi nyingine ni Nyeupe

Beno Ngassa mdogo wa Mrisho Ngassa anayekipiga Tanzania Prisons

Miongoni mwa viungo wa pembeni wanaofanya vizuri ni Benodict Khalfan Ngassa ambaye amekuwa akifanya vizuri. Ngassa ambaye ni mtoto wa mchezaji wa zamani wa Pamba Jiji na Simba SC, Khalfan Ngassa, pia ni mdogo wa kiungo mshambuliaji wa zamani wa Yanga, Simba na Azam, Mrisho Ngassa anatajwa ni mmoja kati ya wachezaji wanaotazamiwa kufanya makubwa siku za usoni. Mambo Uwanjani Blog itawaletea Makala maalum ya kiungo huyo hatari ambaye ndoto zake ni kufuata nyayo za kaka yake Mrisho Ngassa. Beno Ngassa