Na Prince Hoza
DIRISHA kubwa la usajili la msimu uliopita klabu ya Simba SC ilifanya usajili mkubwa ambao ulitazamwa kama sehemu ya kujenga kikosi upya, ni kweli Simba ilianza kwa kumleta kocha mpya Fadlu David's raia wa Afrika Kusini.
Lakini pia iliachana na wachezaji wake ambao wengine iliwasajili msimu juzi, kwa maana kwamba wachezaji ambao waliachwa msimu jana walisajiliwa msimu juzi, na hiyo yote imetokana na skauti mbaya iliyofanywa na waliokuwa wanasimamia usajili.
Kumaliza kwenye nafasi ya tatu na kupata tiketi ya kushiriki michuano ya kombe la Shirikisho barani Afrika, kuliwafanya viongozi wa Simba kuamua kufumua kikosi na kusajili wachezaji wapya pamoja na Mkuu wa benchi la ufundi.
Dirisha kubwa la msimu jana Simba ilifanya usajili mkubwa ambao ulipigiwa hesabu kwamba timu itakuwa moto wa kuotea mbali, ni kweli Simba waliamua kuweka kambi nchini Misri ambapo lengo nikuwapa maandalizi wachezaji wake.
Na waliporudi kwenye ligi walianza vizuri na timu kurudisha matumaini kwa mashabiki wake waliopoteza Imani kutokana na kufanya vibaya msimu juzi na kuambulia nafasi ya tatu.
Simba ilionesha ushindani mkubwa kwenye ligi hiyo na kupelekea ushindani dhidi ya watani zake Yanga, kitendo cha Simba kumaliza ligi katika nafasi ya pili na kupata tiketi ya kushiriki michuano ya Ligi ya mabingwa msimu ujao ni dalili tosha kwamba waliingia kushindana.
Lakini pia Simba ilifika fainali ya kombe la Shirikisho Afrika ambapo walikutana na RS Berkane ya Morocco ambapo kwa bahati mbaya ilipoteza fainali hiyo kwa kufungwa ugenini 2-0 na kutoka sare nyumbani ya 1-1.
Kwa kifupi Simba ilifanikiwa zaidi tofauti na msimu juzi, lakini watani zao Yanga ambao usajili wao haukuwa mkubwa kama ilivyo Simba, ilifanikiwa kutwaa ubingwa wa Ligi Kuu bara ikiwa ni kwa mara ya nne mfululizo.
Yanga pia imeendelea kushinda makombe yote makubwa hapa nchini kama Ngao ya Jamii na kombe la CRDB, msimu uliopita Yanga wamekuwa na bahati nzuri kwani wamechukua na kombe la Muungano, huku pia wakianza kutwaa kombe la Toyota Cup walilolipata nchini Afrika Kusini walipoalikwa.
Kimahesabu ya kawaida kati ya Yanga na Simba nani aliyefanikiwa zaidi unaweza kusema Yanga kwa sababu wametwaa makombe matano likiwemo la Ligi Kuu bara, ambalo hutoa bingwa wa nchi.
Ndipo viongozi wa Simba walipoamua kuuchungulia usajili wao walioufanya msimu uliopita na kubaini haukuwa mzuri moja kwa moja, baadhi ya wachezaji hawakuwa kwenye kiwango bora na Simba ilibebwa na ukubwa wake wa jina.
Wachezaji wapya waliosajiliwa msimu uliopita wamejikuta wakipewa mkono wa kwaheri au thank you, viongozi wa Simba wameendelea kutumia kauli zile zile tunatengeneza kikosi, tofauti ya msimu uliopita na ujao, kwamba Simba imegeukia Afrika Kusini.
Wekundu hao wa Msimbazi, wamejikuta Afrika Kusini na kuwasajili wachezaji wawili ambao ni Rushine De Reuch na Maena wote wakitokea klabu ya Mamelodi Sundown's, mbali na hapo Simba imeendelea kusajili wachezaji kutoka sehemu waliyozoea.
Naona Simba wanarudia yale yale ya msimu uliopita, kwasababu gani natamka maneno hayo, ni kwamba wachezaji wapya wanaosajiliwa waliowengi wanapewa mkataba wa mwaka mmoja huku kukiwa na ya kuongezwa mwaka mmoja tena pindi atakapofanya vizuri.
Ina maana viongozi wa Simba hawajiamini na wachezaji anaowasajili, kuwapa mikataba mifupi watajiingiza kwenye shida pindi msimu unapomalizika kwani wachezaji karibu wengi watakuwa wamemaliza mikataba yao, wasiwasi walionao ni kwamba wachezaji inaowasajili huenda ni dhaifu kama wa msimu uliopita ingawa matokeo ya uwanjani hayapimi ubora wao.
ALAMSIKI