Ruka hadi kwenye maudhui makuu

ANAYEKUMBUKWA: JUMA NASSORO PONDAMALI "MENSAH", ALIKUWA KIPA NWENYE VITUKO LANGONI

Na Prince Hoza, DAR ES SALAAM

KATIKA historia ya magolikipa hapa nchini wapo wengi kama vile Peter Manyika (Senior), Chachala Muya, Kichochi Lemba, Abdul Kipyenga, Spear Mbwembwe, Issa Manofu na wengineo ambao walitaka kumuiga Juma Pondamali 'Mensah' kwa vituko na mbwembwe zake akiwa langoni, lakini hawakumfikia hata robo yake.

Pondamali alikuwa ni wa aina ya kipekee ndani ya nchi hii ambaye kwa sasa ndiyo anawanoa makipa takribani wote wa mabingwa wa soka Tanzania bara Yanga Sc inayonolewa na Mholanzi Hans Van der Pluijm na msaidizi wake Juma Mwambusi.

Achana na yote, Pondamali anashikilia rekodi ya utukutu, kipa huyo alifungiwa mara tano, na pia mara nne mapambano yalivunjika, Pondamali alizaliwa mwaka 1957 jijini Dar es Salaam katika Hospitali ya Ocean Road.

Pondamali alipata masomo yake akianzia shule ya msingi Mlimani na baadaye Karume kabla ya elimu yake ya sekondari kuipata Mzizima muda wote huo wa utoto wake soka likiwa ndani ya damu yake.

KOCHA MZUNGU AMWIBUA JANGWANI

Kocha raia wa Romania Victor Stanculescu mwanzoni mwa miaka ya 70 baada ya kuona wachezaji wa Yanga umri wao unasogea aliita watoto wenye vipaji wenye umri wa Kids yaani miaka 14/15 ili waje wachukue nafasi za wakongwe.

Na ndipo walipojitokeza watoto takribani mia na kupatikana wachache akina Mohamed Mkweche, Adolf Richard, Kassim Manara, Mohamed Tostao, Gordian Mapango, Juma Pondamali na wengineo ambao kwa maelezo ya Victor aliwatabiria kuwa wote lazima watacheza timu ya taifa na ndicho hatimaye kilitokea.

Pondanali na wenzake walipandishwa hadi kikosi cha pili na baadaye mwaka 1974 walipandishwa hadi kikosi cha kwanza na Pondamali akiwa kipa wa tatu akifuatiwa na Muhidin Fadhil na Elias Michael na kutengeneza mziki mzito ndani ya vijana wa Jangwani na walifanya vizuri mwaka 1974 kwa kuwafunga mahasimu zao Simba.

Mwaka uliofuatiwa wakachukua ubingwa wa Klabu bingwa Afrika mashariki na kati na balaa likitokea katika mashindano ya Klabu bingwa Afrika na kutolewa na Enugu Rangers ya Nigeria.

YANGA YAMEGUKA NA KUUNDWA PAN AFRICAN

Matatizo ya wanachama kufuata mkumbo na kutopima mambo, wakamsikiliza kocha Mzaire Tambwe Leya na kuwapuuza wachezaji kwa kila jambo ambalo Tambwe aliwaambia baada ya ile mechi ya kwanza kule Nigeria kutoka sare, Kocha aliapa kuwa ni lazima wataiondosha katika mashindano Enugu na baada ya kutolewa akashusha lawama kwa wachezaji.

Tambwe Leya aliwalaumu akina Boy Idd, Sunday Manara, Omary Kapera, Gibson Sembuli kuwa wameihujumu timu kwahiyo wanachama waamue moja atoke yeye au wachezaji na ndipo wachezaji walipoamua kutimka kwa kuzingatia kuwa hawakuona kosa lao.

Wakubwa wote wakaenda kuunda timu inayoitwa Nyota Afrika ya Morogoro na wale waliokuwa watoto wakajiunga na Pilsner ya Dar es Salaam na baada ya mwaka akina Sembuli wakarudi kuungana na vijana wao ambao ndio walikuwa moto wa kuotea mbali na kuunda Pan Africans kwa masharti kuwa wote vijana wapewe ajira, na kweli vijana wote waliajiliwa kwenye kiwanda cha madawa hivyo ndivyo ilivyounda Pan ikiwa chini ya mzee Tabu Mangala na Shiraz Sharif.

MTUKUTU AKIWA UWANJANI, MPOLE AKIWA NJE YA UWANJA.

Kama kuna watu waliokuwa wakorofi ndani ya uwanja na wapole nje ya uwanja basi Juma Pondamali alikuwa habari nyingine, hawa akina Haruna Moshi 'Boban', Juma Nyosso, Juma Kaseja na wengineo wanasingiziwa tu.

Pondamali aliwahi kufungisha goli kwa makusudi halafu akasimama kumsubiria beki mkorofi Fred Minziro enzi hizo akiwa nahodha wa Yanga, Minziro alionekana akilalanimika lakini hakuweza kumfikia Pondamali kwani angeweza kuchapwa makonde , kipa huyo alikuwa mwanakareti mzuri.

Pondamali ndiye kipa pekee hadi sasa mwenye historia ya kucheza fainali za mataifa Afrika mwaka 1981 nchini Nigeria.

Yapo mengi yanayomuhusu kipa huyo ila sitaweza kuyaeleza yote leo tusubiri siku nyingine kama hii ya leo

Juma Pondamali kipa mwenye vituko aliyetokea miaka ya nyuma

Machapisho maarufu kutoka blogu hii

HISTORIA YA TIMU YA MASHUJAA YA KIGOMA, KUMBE NI SHEA YA JESHI NA WANANCHI

Timu inaitwa Mashujaa Lake Tanganyika FC ( Mashujaa FC ) ilianza rasmi kampeni yake ya kupanda Ligi Kuu tarehe 29/9/2018 na imepanda Ligi Kuu 25/06/2023 miaka mitano ya kupambana kwenye Ligi Daraja la kwanza Championship. Timu hii inaendeshwa kwa ushirikiano wa pande mbili kati ya Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) na Halmashauri ya Manispaa ya Kigoma Ujiji kwa niaba ya Wananchi wa Kigoma. Muelewe hapa maana wengi wanasema ni timu ya Jeshi asilimia 100% Nembo ya timu ni Sokwe Dume, Shujaa wa Hifadhi za Gombe na Mahale zilizopo mkoani Kigoma. Rangi ya kwanza ya jezi ya timu (first kit) ni hiyo hapo chini na kwenye nembo ya timu ni rangi za tunda la michikichi (mawese ). Hii kama njano ni mawese yaliyoganda na huo wekundu ni mawese ya moto. Ukishika tunda la Mse juu utaona wekundu na ukikata katikati utaona njano. Nyeupe ni ‘nazi’ ya Mse hizi ni alama za utajiri wa Kigoma Jezi nyingine ni blue inayowakilisha Ziwa Tanganyika na Jezi nyingine ni Nyeupe

MAKALA: SIMBA NI TIMU YA KWANZA TANZANIA KUINGIA NUSU FAINALI AFRIKA

Na Prince Hoza AFISA Habari wa klabu ya Yanga SC Ally Shabani Kamwe alidiriki kuudanganya umma wa wapenzi wa soka hapa nchini kwamba hakuna timu yoyote hapa Tanzania kuwahi kuingia hatua ya nusu fainali ya vilabu Afrika. Kamwe alisema timu yake ya Yanga itakuwa timu ya kwanza nchini kuingia nusu fainali ya Afrika, Yanga ilikuwa inakaribia kabisa kutinga nusu fainali ya kombe la Shirikisho barani Afrika. Yanga ilianza vizuri ikiwa ugenini baada ya kuilaza mabao 2-0 timu ya Rivers United ya Nigeria, hivyo ilikuwa inasubiria mchezo wa marudiano uliofanyika uwanja wa kumbukumbu ya Benjamin Mkapa jijini Dar es Salaam. Kwa vyovyote Yanga walikuwa na uhakika wa kutinga nusu fainali kwani walihitaji sare yoyote ama ushindi wa aina yoyote. Hapo ndipo Afisa Habari wa Yanga, Ally Kamwe aliamua kupiga vijembe kwa watani zake Simba SC na kuipotosha jamii kwa kudai kwamba Yanga itakuwa timu ya kwanza Tanzania kuingia nusu fainali ya Afrika. Kamwe ameifuta hadi rekodi ya Simba kuwa timu ya kwanza Tan...

Mabululu ni wa Simba SC

Simba wameweka donge nono kunasa saini ya mshambuliaji Agostinho Cristovan Paciencio Mabululu anayekipiga Al Tripoli ya Libya Ili ajiunge na Wekundu hao wa Msimhazi. Simba wamefanya mazungumzo ya moja kwa moja na wakala wa Mabululu na mchezaji mwenyewe na wako tayari kulipa kiasi cha juu zaidi kunasa saini ya mshambuliaji huyo hatari zaidi Simba wanahitaji kumalizana na mshambuliaji huyo badala ya kumaliza fainali ya kombe la Shirikisho, tayari Crecentius Magori yuko nyuma ya mpango huo kuhakikisha Simba ijayo inatisha. Mbali na Mabululu, Simba pia inahitaji Saini ya kiungo mshambuliaji wa Azam FC Feisal Salum "Feitoto" ambaye pia amewahi kuichezea Yanga SC