Ruka hadi kwenye maudhui makuu

UBINGWA WA AZAM YAIZIMA REKODI YA SIMBA

Timu ya Azam ambayo juzi ilitwaa ubingwa wa Tanzania Bara kwa msimu wa 2013/14, imeweka rekodi saba kwenye medani ya soka nchini.

Azam iliifunga Mbeya City mabao 2-1 kwenye uwanja wa Sokoine na kuweka rekodi ya kuwa timu pekee iliyoifunga timu hiyo kwenye uwanja wake wa nyumbani.

Awali, Mbeya City ilikuwa haijawahi kufungwa kwenye uwanja wake wa nyumbani kabla ya rekodi yake kuvunjwa na Azam.


Mabingwa hao wameifikia pia rekodi ya Simba ya kutwaa ubingwa bila ya kupoteza mechi ya msimu wa 2009/10 na sasa wanafukuzia rekodi nyingine ya 'Wekundu wa Msimbazi' ya kumaliza msimu bila ya kupoteza mechi wakati watakapowakabili JKT Ruvu katika mechi yao ya mwisho ya msimu.

Mbali na hilo, pia wameweka rekodi ya kuwa timu ya tisa kutwaa ubingwa wa Tanzania Bara tangu ligi hiyo ilipoanza.

Azam pia imekuwa ni timu ya saba kutwaa ubingwa huo nje ya miamba wawili wa soka nchini ambao wamekuwa wakipokezana ubingwa huo, Simba na Yanga.

Timu nyingine ambazo zimeshawahi kufanya hivyo, nazo ni Cosmopolitan ya Dar es salaam mwaka 1967, Mseto Sports ya Morogoro (1975), Pan African (1982), Tukuyu Stars (1986), Coastal Union (1988) na Mtibwa Sugar mwaka 1999 na 2000.

Rekodi nyingine ni kuwa timu ya tano kutoka jijini Dar es Salaam kutwaa ubingwa wa Bara, ikizifuata timu za Simba, Yanga, Cosmopolitan na Pan African.

Lakini vile vile Azam imekuwa ni timu ya kwanza kutoka nje ya Manispaa ya Ilala kutwaa ubingwa kwani timu za Simba, Yanga, Cosmopolitan na Pan African zinatoka Ilala, huku yenyewe ikitokea Temeke.

Vile vile imekuwa ni timu ya pili ya kampuni kutwaa ubingwa nchini baada ya Mtibwa Sugar kufanya hivyo mwaka 1999 na 2000.

Timu hiyo imetwaa ubingwa kwa pointi 59 ambazo hazitafikiwa na timu yoyote kwenye mechi ya kuhitimisha Ligi Kuu Jumamosi.

Wakati huo huo, Sanula Athanas, anaripoti kuwa wadhamini wakuu wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara (VPL), Kampuni ya Mawasiliano ya Vodacom Tanzania, wameipongeza Azam FC kwa kutwaa ubingwa wa ligi hiyo msimu huu ikiwa ni mara ya kwanza tangu ipande miaka saba iliyopita.

Azam inayonolewa na Mcameroon Joseph Omog ilitwaa ubingwa huo juzi baada ya kuifunga Mbeya City 2-1 katika raundi ya 25 ya ligi hiyo na kufikisha pointi 59 ambazo haziwezi kufikiwa na timu yoyote msimu huu.

Mara tu baada ya kumalizika kwa mechi hiyo kwenye Uwanja wa Kumbukumbu ya Sokoine mjini Mbeya juzi, Meneja Uhusiano wa Nje wa kampumi hiyo, Salum Mwalim alisema wameridhishwa na kiwango cha Azam FC pamoja na timu zote zinazoshiriki katika ligi na hivyo wanawapongeza kwa dhati timu hiyo kutwaa taji.

"Tunawapongeza Azam kwa kuwa bingwa mpya wa VPL kwa sababu wamekabiliana vema na mikikimikiki ya ligi, hivyo ubingwa wao haukuwa mwepesi kuupata kutokana na ushindani uliokuwapo kwa timu zote shiriki," alisema Mwalim.

"Tunaamini ubingwa huu wa Azam utaifanya ligi msimu ujao kuwa ngumu zaidi kwani timu za Yanga na Simba ambazo zimekuwa zikipokezana ubingwa tangu 2001 zitataka kurudisha heshima yao na nyingine zikipata nguvu kwa kuwa yoyote inaweza kuwa bingwa, na hilo likitokea ubora wa ligi yetu utazidi kupaa," alisema zaidi Mwalim.

Alisema Azam watakabidhiwa kombe lao la ubingwa Jumamosi kwenye uwanja wao wa nyumbani, Chamazi jijini Dar es Salaam wakati wa mechi yao ya mwisho dhidi ya JKT Ruvu.

Aidha Mwalim amezipongeza timu zote 14 zilizoshiriki ligi hiyo kwa kujituma na kutoa changamoto katika kila mechi jambo lililofanya bingwa kutopatikana kwa urahisi na mapema.

Machapisho maarufu kutoka blogu hii

HISTORIA YA TIMU YA MASHUJAA YA KIGOMA, KUMBE NI SHEA YA JESHI NA WANANCHI

Timu inaitwa Mashujaa Lake Tanganyika FC ( Mashujaa FC ) ilianza rasmi kampeni yake ya kupanda Ligi Kuu tarehe 29/9/2018 na imepanda Ligi Kuu 25/06/2023 miaka mitano ya kupambana kwenye Ligi Daraja la kwanza Championship. Timu hii inaendeshwa kwa ushirikiano wa pande mbili kati ya Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) na Halmashauri ya Manispaa ya Kigoma Ujiji kwa niaba ya Wananchi wa Kigoma. Muelewe hapa maana wengi wanasema ni timu ya Jeshi asilimia 100% Nembo ya timu ni Sokwe Dume, Shujaa wa Hifadhi za Gombe na Mahale zilizopo mkoani Kigoma. Rangi ya kwanza ya jezi ya timu (first kit) ni hiyo hapo chini na kwenye nembo ya timu ni rangi za tunda la michikichi (mawese ). Hii kama njano ni mawese yaliyoganda na huo wekundu ni mawese ya moto. Ukishika tunda la Mse juu utaona wekundu na ukikata katikati utaona njano. Nyeupe ni ‘nazi’ ya Mse hizi ni alama za utajiri wa Kigoma Jezi nyingine ni blue inayowakilisha Ziwa Tanganyika na Jezi nyingine ni Nyeupe

MAKALA: SIMBA NI TIMU YA KWANZA TANZANIA KUINGIA NUSU FAINALI AFRIKA

Na Prince Hoza AFISA Habari wa klabu ya Yanga SC Ally Shabani Kamwe alidiriki kuudanganya umma wa wapenzi wa soka hapa nchini kwamba hakuna timu yoyote hapa Tanzania kuwahi kuingia hatua ya nusu fainali ya vilabu Afrika. Kamwe alisema timu yake ya Yanga itakuwa timu ya kwanza nchini kuingia nusu fainali ya Afrika, Yanga ilikuwa inakaribia kabisa kutinga nusu fainali ya kombe la Shirikisho barani Afrika. Yanga ilianza vizuri ikiwa ugenini baada ya kuilaza mabao 2-0 timu ya Rivers United ya Nigeria, hivyo ilikuwa inasubiria mchezo wa marudiano uliofanyika uwanja wa kumbukumbu ya Benjamin Mkapa jijini Dar es Salaam. Kwa vyovyote Yanga walikuwa na uhakika wa kutinga nusu fainali kwani walihitaji sare yoyote ama ushindi wa aina yoyote. Hapo ndipo Afisa Habari wa Yanga, Ally Kamwe aliamua kupiga vijembe kwa watani zake Simba SC na kuipotosha jamii kwa kudai kwamba Yanga itakuwa timu ya kwanza Tanzania kuingia nusu fainali ya Afrika. Kamwe ameifuta hadi rekodi ya Simba kuwa timu ya kwanza Tan...

Mabululu ni wa Simba SC

Simba wameweka donge nono kunasa saini ya mshambuliaji Agostinho Cristovan Paciencio Mabululu anayekipiga Al Tripoli ya Libya Ili ajiunge na Wekundu hao wa Msimhazi. Simba wamefanya mazungumzo ya moja kwa moja na wakala wa Mabululu na mchezaji mwenyewe na wako tayari kulipa kiasi cha juu zaidi kunasa saini ya mshambuliaji huyo hatari zaidi Simba wanahitaji kumalizana na mshambuliaji huyo badala ya kumaliza fainali ya kombe la Shirikisho, tayari Crecentius Magori yuko nyuma ya mpango huo kuhakikisha Simba ijayo inatisha. Mbali na Mabululu, Simba pia inahitaji Saini ya kiungo mshambuliaji wa Azam FC Feisal Salum "Feitoto" ambaye pia amewahi kuichezea Yanga SC