Ruka hadi kwenye maudhui makuu

SIMBA KIMENUKA, YAFUMULIWA TENA NA COASTAL UNION

Kikosi cha Coastal Union kilichofanyiwa mabadiliko kikiwaacha nje nyota wa zamani wa Simba akiwamo beki Juma Nyosso na kiungo Haruna Moshi 'Boban', jana kiliwashangaza Wekundu wa Msimbazi kwa kipigo kingine kisichotarajiwa cha 1-0 kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam, huku Azam FC ikibaki kileleni kufuatia ushindi wa 1-0 dhidi ya JKT Oljoro.

Kilikuwa ni kipigo cha nne kwa Simba msimu huu kilichowaacha Wekundu hao katika nafasi ya nne ya msimamo wakiwa na pointi 36, wakati Azam walijiimarisha kileleni kwa kufikisha pointi 47, nne juu ya Yanga iliyo katika nafasi ya pili. Yanga imecheza mechi moja pungufu.

Azam walipata goli lao la pekee kupitia kwa John Bocco 'Adebayor' katika dakika ya 71 kwenye Uwanja wa Azam Complex, ambako timu hiyo ambayo haijapoteza mchezo hata mmoja ilionekana kama ingedondosha pointi mbili baada ya kipindi cha kwanza kumalizika matokeo yakiwa 0-0.


Kwenye Uwanja wa Taifa, Coastal walifunga goli lao katika dakika ya 44 kupitia kwa Hamad Juma aliyetumia vyema makosa ya beki wa Simba, Omary Salum, ambaye alimruhusu akauwahi mpira na kupiga shuti lililotinga wavuni.

Mpira ulianza kwa utulivu lakini katika dakika ya 8 beki wa Coastal Abdi Banda aliokoa kishujaa shuti la mshambuliaji Mrundi Amisi Tambwe lililokuwa linaelekea katika lango lao.

Katika dakika hizo za kwanza ambazo Simba walicheza vizuri, Coastal walikuwa makini kuhakikisha hawaruhusu goli la mapema. Katika dakika ya 17, Mbwana Hamis aliokoa krosi ya winga wa Simba, Ramadhani Singano 'Messi' na kuikosesha Simba nafasi ya kufunga na katika dakika ya 23 winga wa Simba, Haruna Chanongo alipiga pembeni na kupoteza pasi nzuri ya Omary Salum.

Wageni walicharuka kwa shambulizi katika dakika ya 23 lakini kipa wa Simba, Ivo Mapunda aliwahi kudaka mpira wa kichwa uliopigwa na Ally Nassor kutokea ndani ya boksi na kuikosesha Coastal nafasi ya kufunga.

Simba walikaribia kufunga katika dakika ya 73 lakini shuti la Jonas Mkude liligonga nguzo ya lango na kurejea uwanjani.

Vikosi vilikuwa; Simba: Ivo Mapunda, Haruna Shamte/ Christopher Edward (dk.62), Issa Rashid 'Baba Ubaya', Joseph Owino, Donald Musoti, Henry Joseph, Omari Salum/ William Lucian (dk.46), Jonas Mkude, Haruna Chanongo, Amisi Tambwe na Ramadhani Singano 'Messi'.

Kocha wa Coastal Union, Yusuf Chipo alielezea furaha yake kwa ushindi huo dhidi ya timu kubwa huku akisema ulichangiwa na mabadiliko ya kikosi aliyoyafanya dhidi ya kile kilichopigwa 4-0 dhidi ya Azam FC katika mechi yao iliyopita.

Alisema Simba ilicheza vyema katika dakika za kwanza lakini walipowafunga goli walichanganyikiwa na kushindwa kurejea mchezoni.

Chipo, ambaye ushindi uliifanya timu yake ifikishe pointi 29 na kukaa katika nafasi ya saba, alisema anataka kumaliza katika nafasi bora zaidi msimu huu.
Katika mechi ya mzunguko wa kwanza baina ya Simba na Coastal kwenye Uwanja wa Mkwakwani, Tanga timu hizo zilitoka 0-0.

Katika kuonyesha fadhaa, winga Singano alidaiwa kupiga teke kioo cha mlango wa kuingilia katika chumba cha kuvalia cha Simba na kukivunja.

Coastal Union: Fikirini Selemani, Hamadi Juma/ Ayoub Masoud (dk.60), Abdi Banda, Yusuf Chuma, Mbwana Hamis, Razack Khalfan, Ally Nassor/ Mohammed Mtindi (dk.35), Behewa Sembwana, Seleimani Kassim 'Selembe'/ Marcus Ndeheli (dk.75), Daniel Lyanga na Kenneth Masumbuko.

Katika matokeo mengine ya jana, Ruvu Shooting iliifunga Ashanti 2-0 kupitia magoli mawili ya Elias Maguri katika dakika ya 6 na 63, huku Mgambo ikitoka sare ya 1-1 dhidi ya Mtibwa Sugar kwenye Uwanja wa Mkwakwani Tanga.


Machapisho maarufu kutoka blogu hii

HISTORIA YA TIMU YA MASHUJAA YA KIGOMA, KUMBE NI SHEA YA JESHI NA WANANCHI

Timu inaitwa Mashujaa Lake Tanganyika FC ( Mashujaa FC ) ilianza rasmi kampeni yake ya kupanda Ligi Kuu tarehe 29/9/2018 na imepanda Ligi Kuu 25/06/2023 miaka mitano ya kupambana kwenye Ligi Daraja la kwanza Championship. Timu hii inaendeshwa kwa ushirikiano wa pande mbili kati ya Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) na Halmashauri ya Manispaa ya Kigoma Ujiji kwa niaba ya Wananchi wa Kigoma. Muelewe hapa maana wengi wanasema ni timu ya Jeshi asilimia 100% Nembo ya timu ni Sokwe Dume, Shujaa wa Hifadhi za Gombe na Mahale zilizopo mkoani Kigoma. Rangi ya kwanza ya jezi ya timu (first kit) ni hiyo hapo chini na kwenye nembo ya timu ni rangi za tunda la michikichi (mawese ). Hii kama njano ni mawese yaliyoganda na huo wekundu ni mawese ya moto. Ukishika tunda la Mse juu utaona wekundu na ukikata katikati utaona njano. Nyeupe ni ‘nazi’ ya Mse hizi ni alama za utajiri wa Kigoma Jezi nyingine ni blue inayowakilisha Ziwa Tanganyika na Jezi nyingine ni Nyeupe

MAKALA: SIMBA NI TIMU YA KWANZA TANZANIA KUINGIA NUSU FAINALI AFRIKA

Na Prince Hoza AFISA Habari wa klabu ya Yanga SC Ally Shabani Kamwe alidiriki kuudanganya umma wa wapenzi wa soka hapa nchini kwamba hakuna timu yoyote hapa Tanzania kuwahi kuingia hatua ya nusu fainali ya vilabu Afrika. Kamwe alisema timu yake ya Yanga itakuwa timu ya kwanza nchini kuingia nusu fainali ya Afrika, Yanga ilikuwa inakaribia kabisa kutinga nusu fainali ya kombe la Shirikisho barani Afrika. Yanga ilianza vizuri ikiwa ugenini baada ya kuilaza mabao 2-0 timu ya Rivers United ya Nigeria, hivyo ilikuwa inasubiria mchezo wa marudiano uliofanyika uwanja wa kumbukumbu ya Benjamin Mkapa jijini Dar es Salaam. Kwa vyovyote Yanga walikuwa na uhakika wa kutinga nusu fainali kwani walihitaji sare yoyote ama ushindi wa aina yoyote. Hapo ndipo Afisa Habari wa Yanga, Ally Kamwe aliamua kupiga vijembe kwa watani zake Simba SC na kuipotosha jamii kwa kudai kwamba Yanga itakuwa timu ya kwanza Tanzania kuingia nusu fainali ya Afrika. Kamwe ameifuta hadi rekodi ya Simba kuwa timu ya kwanza Tan...

Mabululu ni wa Simba SC

Simba wameweka donge nono kunasa saini ya mshambuliaji Agostinho Cristovan Paciencio Mabululu anayekipiga Al Tripoli ya Libya Ili ajiunge na Wekundu hao wa Msimhazi. Simba wamefanya mazungumzo ya moja kwa moja na wakala wa Mabululu na mchezaji mwenyewe na wako tayari kulipa kiasi cha juu zaidi kunasa saini ya mshambuliaji huyo hatari zaidi Simba wanahitaji kumalizana na mshambuliaji huyo badala ya kumaliza fainali ya kombe la Shirikisho, tayari Crecentius Magori yuko nyuma ya mpango huo kuhakikisha Simba ijayo inatisha. Mbali na Mabululu, Simba pia inahitaji Saini ya kiungo mshambuliaji wa Azam FC Feisal Salum "Feitoto" ambaye pia amewahi kuichezea Yanga SC