Ruka hadi kwenye maudhui makuu

YANGA YAIPISHA AZAM KILELENI, KIPRE TCHETCHE HATARI.

Mabingwa Yanga walishikwa kwa sare ya 0-0 ugenini mkoani Tanga dhidi ya Coastal Union na kushuhudia wakitema uongozi wa Ligi Kuu ya Tanzania Bara baada ya Azam FC kushinda 1-0 dhidi ya Rhino Rangers na kushika usukani wa ligi.

Mbeya City ambao waliianza siku ya jana wakiwa na pointi 30 sawa na Azam, nao walidondosha pointi mbili jana kufuatia sare ya 1-1 ugenini Ruvu Shooting kwenye Uwanja wa Mabatini.

Matokeo hayo yalimaanisha kwamba Azam sasa wako kileleni mwa msimamo wakiwa na pointi 33, moja juu ya Yanga walio katika nafasi ya pili, huku Mbeya City wakibaki katika nafasi yao ya tatu wakiwa na pointi 31.


Simba walio katika nafasi ya nne wakiwa na pointi 27, wanayo fursa ya kusogea hadi pointi tatu nyuma ya vinara Azam kwa ushindi dhidi ya JKT Oljoro kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam kesho.   

Mfungaji Bora wa Ligi Kuu Bara msimu uliopita Kipre Tchetche alifunga bao lake la 9 katika dakika ya 31 jana na hivyo kubakisha goli moja kumfikia kinara Amisi Tambwe wa Simba wakati alipoisaidia Azam kupanda kileleni kwenye Uwanja wa Azam Complex. 

Ruvu Shooting walitangulia kupata goli kupitia kwa Jerome Lambele katika dakika ya 4 lakini Mbeya City ambayo pamoja na Azam ndizo timu pekee ambazo hazijapoteza mechi hadi sasa, ilisawazisha kupitia kwa Deus Kaseke dakika kumi baadaye.

Mkoani Tanga, Yanga walianza kwa kasi wakapata kona tatu ndani ya dakika tano za mwanzo lakini hazikuzaa matunda kutokana na umahiri wa kipa wao wa zamani Shaban Kado aliyepangua pia mashuti ya winga Mrisho Ngasa na kiungo Haruna Niyonzima 'Fabregas'.

Katika dakika ya 29 mpira ulilazimika kusimama kwa dakika moja kupisha uokotaji wa chupa za maji zilizorushwa na mashabiki walioaminika kuwa Yanga waliochukia baada ya refa msaidizi namba moja John Kanyenye wa Iringa kukataa kuwapa penalti baada ya mshambuliaji Mrundi Didier Kavumbagu kumnawisha mpira beki wa Coastal, Juma Nyoso ndani ya boksi. Hata hivyo, Kavumbagu alifanya faulo kabla ya tukio hilo kwani alinyanyua mguu wakati Nyoso akitaka kupiga kichwa.

Dakika tisa baadaye, mashabiki wa Coastal walijibu mapigo kwa kurusha chupa za maji langoni mwa Yanga baada ya timu yao kufanya shambulizi kali la kushtukiza. Mpira pia ulisimama kwa dakika moja kupisha uokotaji wa wa chupa hizo.

Yanga walifanya mashambulizi hatari 13 kipindi cha kwanza yaliyozaa kona nane huku wenyeji wao wakifanya mashambulizi matatu makali ya kushtukiza na yaliyompa wakati mgumu kipa Deogratius Munishi 'Dida' kuokoa.

Coastal walibadilika kwa kiasi kikubwa kipindi cha pili wakisaidiwa na upepo mkali uliokuwa unavuma kutoka Kaskazini kuelekea lango la Yanga na kuwachanganya wachezaji wa Yanga hadi kufikia hatua Cannavaro kumsukuma Niyonzima katika dakika ya 73.

Baada ya mechi hiyo, kocha wa Yanga, Hans der Pluijm, alisema: "Tulipoteza mechi kipindi cha kwanza tuliposhindwa kupata bao licha ya kutengeneza nafasi nyingi. Kipindi cha pili tulishindwa kucheza mpira mzuri kutokana na upepo mkali."

Kocha wa Coastal, Mkenya Yusuph Chiko alisema: "Ni jambo jema tumepata pointi na hatujapoteza mechi tulicheza vizuri kipindi cha pili lakini bado tuna upungufu katika kuzitumia nafasi tunazotengeneza. Tutalifanyia kazi suala hili."

Vikosi Tanga vilikuwa; Coastal Union: Shaban Kado, Hamad Juma, Abdi Banda, Juma Nyoso, Mbwana Bakari, Jerry Santo, Daud Liyanga, Chrispin Odula, Lutimba Yayo/ Mohamed Miraji (dk. 88), , Haruna Moshi na Keneth Masumbuko/ Mohamed Sudi (dk. 78).

Yanga: Deogratius Munishi, Mbuyu Twite, Oscar Joshua. Nadir Haroub, Kelvin Yondani, Frank Domayo, Simon Msuva, Haruna Niyonzima, Didier Kavumbagu, Mrisho Ngasa/ Nizar Khalifani (dk. 83) na David Luhende/ Jerry Tegete (dk 66).

Machapisho maarufu kutoka blogu hii

HISTORIA YA TIMU YA MASHUJAA YA KIGOMA, KUMBE NI SHEA YA JESHI NA WANANCHI

Timu inaitwa Mashujaa Lake Tanganyika FC ( Mashujaa FC ) ilianza rasmi kampeni yake ya kupanda Ligi Kuu tarehe 29/9/2018 na imepanda Ligi Kuu 25/06/2023 miaka mitano ya kupambana kwenye Ligi Daraja la kwanza Championship. Timu hii inaendeshwa kwa ushirikiano wa pande mbili kati ya Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) na Halmashauri ya Manispaa ya Kigoma Ujiji kwa niaba ya Wananchi wa Kigoma. Muelewe hapa maana wengi wanasema ni timu ya Jeshi asilimia 100% Nembo ya timu ni Sokwe Dume, Shujaa wa Hifadhi za Gombe na Mahale zilizopo mkoani Kigoma. Rangi ya kwanza ya jezi ya timu (first kit) ni hiyo hapo chini na kwenye nembo ya timu ni rangi za tunda la michikichi (mawese ). Hii kama njano ni mawese yaliyoganda na huo wekundu ni mawese ya moto. Ukishika tunda la Mse juu utaona wekundu na ukikata katikati utaona njano. Nyeupe ni ‘nazi’ ya Mse hizi ni alama za utajiri wa Kigoma Jezi nyingine ni blue inayowakilisha Ziwa Tanganyika na Jezi nyingine ni Nyeupe

MAKALA: SIMBA NI TIMU YA KWANZA TANZANIA KUINGIA NUSU FAINALI AFRIKA

Na Prince Hoza AFISA Habari wa klabu ya Yanga SC Ally Shabani Kamwe alidiriki kuudanganya umma wa wapenzi wa soka hapa nchini kwamba hakuna timu yoyote hapa Tanzania kuwahi kuingia hatua ya nusu fainali ya vilabu Afrika. Kamwe alisema timu yake ya Yanga itakuwa timu ya kwanza nchini kuingia nusu fainali ya Afrika, Yanga ilikuwa inakaribia kabisa kutinga nusu fainali ya kombe la Shirikisho barani Afrika. Yanga ilianza vizuri ikiwa ugenini baada ya kuilaza mabao 2-0 timu ya Rivers United ya Nigeria, hivyo ilikuwa inasubiria mchezo wa marudiano uliofanyika uwanja wa kumbukumbu ya Benjamin Mkapa jijini Dar es Salaam. Kwa vyovyote Yanga walikuwa na uhakika wa kutinga nusu fainali kwani walihitaji sare yoyote ama ushindi wa aina yoyote. Hapo ndipo Afisa Habari wa Yanga, Ally Kamwe aliamua kupiga vijembe kwa watani zake Simba SC na kuipotosha jamii kwa kudai kwamba Yanga itakuwa timu ya kwanza Tanzania kuingia nusu fainali ya Afrika. Kamwe ameifuta hadi rekodi ya Simba kuwa timu ya kwanza Tan...

Mabululu ni wa Simba SC

Simba wameweka donge nono kunasa saini ya mshambuliaji Agostinho Cristovan Paciencio Mabululu anayekipiga Al Tripoli ya Libya Ili ajiunge na Wekundu hao wa Msimhazi. Simba wamefanya mazungumzo ya moja kwa moja na wakala wa Mabululu na mchezaji mwenyewe na wako tayari kulipa kiasi cha juu zaidi kunasa saini ya mshambuliaji huyo hatari zaidi Simba wanahitaji kumalizana na mshambuliaji huyo badala ya kumaliza fainali ya kombe la Shirikisho, tayari Crecentius Magori yuko nyuma ya mpango huo kuhakikisha Simba ijayo inatisha. Mbali na Mabululu, Simba pia inahitaji Saini ya kiungo mshambuliaji wa Azam FC Feisal Salum "Feitoto" ambaye pia amewahi kuichezea Yanga SC