Ruka hadi kwenye maudhui makuu

STARS DHIDI YA KENYA ‘INAYOBEBWA VIBAYA’ NA MAREFA CHALLENGE 2013, PATACHIMBIKA MACHAKOS LEO

TANZANIA Bara ‘Kilimanjaro Stars’, leo inashuka dimbani kwenye Uwanja wa Kenyatta, Machakos, kumenyana na wenyeji, Kenya ‘Harambee Stars’ katika Nusu Fainali ya Kombe la Mataifa ya Afrika Mashariki na Kati, CECAFA Challenge kuanzia saa 7:00 mchana.

Hii ni mara ya pili mfululizo kwa Stars chini ya kocha Mdenmark, Kim Poulsen kufika Nusu Fainali ya michuano hiyo, baada ya mwaka jana pia mjini Kampala, Uganda ambako ilitolewa na wenyeji, Uganda ‘The Cranes’ kwa kufungwa mabao 3-0.

Lakini Kim, amelipa kisasi kwa The Cranes, baada ya Stars kuivua ubingwa Uganda Jumamosi kwa kuitoa kwenye Robo Fainali, Uwanja wa County ya Mombasa, zamani Manispaa kwa penalti 3-2, kufuatia sare ya 2-2 ndani ya dakika 90.

Baada ya kumaliza shughuli hiyo pevu, Kim anakabiliwa na jukumu lingine zito mbele yake, ambalo ni Nusu Fainali dhidi ya Kenya, ambayo imeonekana ‘kubebwa’ mno na marefa hadi sasa katika mashindano haya.


Kenya imekuwa ikipewa penalti katika mechi zote kuanzia hatua ya makundi hadi Robo Fainali na hali hiyo inatarajiwa kwa kiasi kikubwa kuendelea na leo pia Machakos.

Beki wa Azam FC, Joackins Atudo amepiga penalti nne na kufunga tatu hadi sasa, wakati moja alikosa katika mechi ya Kundi A dhidi ya Sudan Kusini.
Habari njema ni kwamba, kipa wa Stars, Ivo Mapunda anaheshimika mno kwa uhodari wa kucheza penalti, lakini pia Wakenya wanamuamini mno Atudo katika upigaji.

Mechi hiyo imeteka hisia za wengi na sababu za Shirikisho la Soka Kenya (FKF) kuipeleka Uwanja wa Kenyatta badala ya Nyayo, Nairobi ni kutokana na imani kwamba watu wa huko huishagilia mno Harambee Stars inapocheza.
 
Wakati Stars iliitoa Uganda, Kenya waliingia Nusu Fainali baada ya kuifunga 1-0 Rwanda ‘Amavubi’ kwa bao la penalti iliyotolewa katika mazingira ya utata iliyopigwa na Atudo kama kawaida.

Kenya ina ukuta imara, safu nzuri ya kiungo, lakini haina makali sana katika safu yake ya ushambuliaji, wakati Tanzania Bara japokuwa itamkosa kiungo wake, Salum Abubakar ‘Sure Boy’ aliyeonyeshwa kadi nyekundu dhidi ya Uganda, bado ina viungo wengine bora wa kuziba pengo hilo.

Kuna chipukizi Hassan Dilunga wa Ruvu Shooting na mkongwe Athumani Iddi ‘Chuji’ wa Yanga, ambao yeyote kati yao Kim anaweza kumpa jukumu la kuziba pengo la kiungo wa Azam FC, Sure Boy.

Stars ina ukuta imara kama ilivyo kwa safu ya kiungo na utamu zaidi ni safu yake ya ushambuliaji inayoundwa na wakali wawili wa TP Mazembe ya DRC, Mbwana Ally Samatta na Thomas Emmanuel Ulimwengu kwa pamoja na Mrisho Khalfan Ngassa wa Yanga.
   
Iwapo hali ya Ngassa haitakuwa imeimarika, hakuna shaka ‘viberenge’ vya Simba SC, Haroun Chanongo na Ramadhani Singano ‘Messi’ mmoja wao anaweza kuchukua nafasi na akafanya kazi nzuri- lakini pia kuna makinda mengine mawili ya Azam FC, Joseph Kimwaga na Farid Mussa pia wanaweza kucheza nafasi hiyo.

Litakuwa pengo kumkosa Ngassa kutokana na uzoefu wake ambao tayari anao hivi sasa kisoka, lakini pia itakuwa nafasi nzuri kwa chipukizi hao kuupambanua uwezo wao, iwapo watapewa nafasi.

Himid Mao amemaliza adhabu ya kadi na baada ya kuwa nje ya Uwanja katika mechi dhidi ya Uganda, leo anarudi kwenye mashindano na litakuwa jukumu la Kim kumchezesha kiraka huyo wa Azam, au kumpanga tena Michael Aidan wa Ruvu Shooting. Nusu Fainali nyingine ni kati ya Zambia na Sudan mjini Mombasa.

Kila la heri Tanzania Bara ‘Kilimanjaro Stars’

Machapisho maarufu kutoka blogu hii

HISTORIA YA TIMU YA MASHUJAA YA KIGOMA, KUMBE NI SHEA YA JESHI NA WANANCHI

Timu inaitwa Mashujaa Lake Tanganyika FC ( Mashujaa FC ) ilianza rasmi kampeni yake ya kupanda Ligi Kuu tarehe 29/9/2018 na imepanda Ligi Kuu 25/06/2023 miaka mitano ya kupambana kwenye Ligi Daraja la kwanza Championship. Timu hii inaendeshwa kwa ushirikiano wa pande mbili kati ya Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) na Halmashauri ya Manispaa ya Kigoma Ujiji kwa niaba ya Wananchi wa Kigoma. Muelewe hapa maana wengi wanasema ni timu ya Jeshi asilimia 100% Nembo ya timu ni Sokwe Dume, Shujaa wa Hifadhi za Gombe na Mahale zilizopo mkoani Kigoma. Rangi ya kwanza ya jezi ya timu (first kit) ni hiyo hapo chini na kwenye nembo ya timu ni rangi za tunda la michikichi (mawese ). Hii kama njano ni mawese yaliyoganda na huo wekundu ni mawese ya moto. Ukishika tunda la Mse juu utaona wekundu na ukikata katikati utaona njano. Nyeupe ni ‘nazi’ ya Mse hizi ni alama za utajiri wa Kigoma Jezi nyingine ni blue inayowakilisha Ziwa Tanganyika na Jezi nyingine ni Nyeupe

MAKALA: SIMBA NI TIMU YA KWANZA TANZANIA KUINGIA NUSU FAINALI AFRIKA

Na Prince Hoza AFISA Habari wa klabu ya Yanga SC Ally Shabani Kamwe alidiriki kuudanganya umma wa wapenzi wa soka hapa nchini kwamba hakuna timu yoyote hapa Tanzania kuwahi kuingia hatua ya nusu fainali ya vilabu Afrika. Kamwe alisema timu yake ya Yanga itakuwa timu ya kwanza nchini kuingia nusu fainali ya Afrika, Yanga ilikuwa inakaribia kabisa kutinga nusu fainali ya kombe la Shirikisho barani Afrika. Yanga ilianza vizuri ikiwa ugenini baada ya kuilaza mabao 2-0 timu ya Rivers United ya Nigeria, hivyo ilikuwa inasubiria mchezo wa marudiano uliofanyika uwanja wa kumbukumbu ya Benjamin Mkapa jijini Dar es Salaam. Kwa vyovyote Yanga walikuwa na uhakika wa kutinga nusu fainali kwani walihitaji sare yoyote ama ushindi wa aina yoyote. Hapo ndipo Afisa Habari wa Yanga, Ally Kamwe aliamua kupiga vijembe kwa watani zake Simba SC na kuipotosha jamii kwa kudai kwamba Yanga itakuwa timu ya kwanza Tanzania kuingia nusu fainali ya Afrika. Kamwe ameifuta hadi rekodi ya Simba kuwa timu ya kwanza Tan...

Mabululu ni wa Simba SC

Simba wameweka donge nono kunasa saini ya mshambuliaji Agostinho Cristovan Paciencio Mabululu anayekipiga Al Tripoli ya Libya Ili ajiunge na Wekundu hao wa Msimhazi. Simba wamefanya mazungumzo ya moja kwa moja na wakala wa Mabululu na mchezaji mwenyewe na wako tayari kulipa kiasi cha juu zaidi kunasa saini ya mshambuliaji huyo hatari zaidi Simba wanahitaji kumalizana na mshambuliaji huyo badala ya kumaliza fainali ya kombe la Shirikisho, tayari Crecentius Magori yuko nyuma ya mpango huo kuhakikisha Simba ijayo inatisha. Mbali na Mabululu, Simba pia inahitaji Saini ya kiungo mshambuliaji wa Azam FC Feisal Salum "Feitoto" ambaye pia amewahi kuichezea Yanga SC