Ruka hadi kwenye maudhui makuu

YANGA YAANGUSHIWA KIPIGO CHA SHARUBELA

Mabingwa watetezi Yanga waliendeleza mwanzo mbaya wa msimu wakati walipokumbana na kipigo cha magoli 3-2 kutoka kwa Azam FC kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam jana.


Matokeo hayo yaliwaacha Yanga wakiwa na pointi 6 baada ya mechi tano, wakitoka sare tatu mfululizo kabla ya kipigo cha jana.

Yanga ambao walianza ligi kwa kishindo wakiikaribisha timu iliyopanda daraja ya Ashanti United kwa magoli 5-1 katika mechi ya ufunguzi wa ligi, jana walitanguliwa kwa goli la sekunde ya 27 tu tangu mechi kuanza lililofungwa na mshambuliaji mrefu John Bocco 'Adebayor'.

Bocco alifunga goli hilo akimalizia kwa kichwa mpira uliobabatizwa na beki Kelvin Yondani wa Yanga aliyekuwa akiokoa mpira wa kichwa cha Brian Umony aliyepokea krosi murua ya winga aliyepandishwa timu ya wakubwa kutoka kikosi cha vijana cha Azam, Farid Musa na kufanya goli la mapema zaidi kufungwa kwenye ligi kuu ya Bara msimu huu.

Baada ya goli hilo kufungwa, Yanga walianza kulisakama kama nyuki lango la Azam huku wakitawala kipindi chote cha kwanza lakini umakini wa kipa Aishi Manula uliiokoa Azam kufungwa mvua ya magoli kwani alipangua mashuti matatu hatari yaliyolenga goli mashuti mawili ya Kavumbagu na Twite yakigonga mwamba.

Hadi mapumziko Azam walikuwa wanaongoza 1-0 huku Joackins Atudo akionyeshwa kadi ya njano na refa Dominic Nyamisana wa Dodoma kwa kupoteza muda

Dakika nne baada ya kuanza kwa kipindi cha pili, mshambuliaji Mrundi Didier Kavumbagu alisawazishia Yanga baada kukokota mpira kutoka katikati ya uwanja na kumlamba chenga kipa Manula kabla ya kuukwamisha mpira wavuni na kuwainua vitini mashabiki wa Yanga ambao walikuwa kimya.

Dakika ya 21 mtokeabenchi Hamis Kiiza, ambaye alikuwa ndiyo kwanza amerejea nchini akitokea kujaribu kucheza soka la kulipwa Uturuki, aliifungia Yanga goli la pili akimalizia kwa mguu wa kulia krosi kali ya Simon Msuva na kuifanya Yanga iwe mbele kwa magoli 2-1.

Azam walisawazisha goli hilo katika dakika ya 70 kupitia kwa mfungaji bora msimu uliopita, Kipre Tchetche, aliyefunga kwa penalti iliyoamuliwa na refa Dominic Nyamisana baada ya kiungo Haruna Niyonzima kushika mpira ndani ya boksi wakati akiokoa krosi ya Kipre Balou. Lilikuwa goli la kwanza kwa Tchetche tangu msimu huu uanze Agosti 24.

Joseph Kimwaga aliyeingia dakika ya 72 kuchukua nafasi ya Faridi Musa, aliifungia Azam goli la tatu na la ushindi baada ya wenyeji hao wa mechi ya jana kufanya shambulizi kali la kushtukiza katika dakika ya 90.

Goli hilo lilikuja sekunde chache tu baada ya Yanga kukosa goli la wazi. Mpira ulianza kwa kipa Manula kupangua kishujaa shuti kali la Simon Msuva kisha wakati Yanga wakionekana kujisahau mpira mrefu ukapigwa kwa winga huyo aliyepandishwa kutoka kikosi cha vijana cha Azam.

Akatulia na kumchambua vyema kipa Ali Mustapha 'Barthez' na kuipa timu yake ushindi wa pili katika mechi tano.

Jukwaa la Simba lililipuka kwa shangwe kufuatia kufungwa kwa goli la tatu ambalo lilishuhudiwa pia na benchi la ufundi la Simba lilikuwapo uwanjani likiongozwa na kocha msaidizi, Jamhuri Kihwelo 'Julio'.

Baada ya mechi hiyo kumalizika kocha wa Azam, Muingereza Stewart Hall alisema "timu bora imeshinda.

Yanga wamecheza vizuri lakini tumewazidi mbinu."
Kocha wa Yanga, Mholanzi Ernie Brandts alisema: "Wachezaji wetu wamecheza vizuri, tumetengeneza nafasi nyingi lakini hatukuwa na bahati. Ligi ni ngumu,t utaendelea kujipanga zaidi."

Hiyo ilikuwa ni mechi ya kwanza kwa Yanga kupoteza msimu huu baada ya kutoka sare tatu mfululizo dhidi ya Coastal Union (nyumbani), Mbeya City na Prisons (ugenini).

Simba wanaendelea kuongoza ligi hiyo wakiwa na pointi 11 baada ya mechi tano.

Katika mechi nyingine za jana, JKT Ruvu walioanza ligi kwa kushinda mechi tatu mfululizo na kuongoza kwa muda msimamo wa ligi hiyo inayodhaminiwa na kampuni ya huduma za simu ya Vodacom Tanzania, jana walikumbana na kichapo cha pili mfululizo cha 1-0 dhidi ya wageni Oljoro JKT kwenye uwanja wa Mabatini, Pwani huku ndugu zao Ruvu Shooting wakipata kipigo kama hicho dhidi ya wenyeji Coastal Union kwenye uwanja wa Mkwakwani jijini Tanga.

Goli la Oljoro dhidi ya JKT Ruvu lilifungwa na Paul Malipesa katika dakika ya 79, wakati goli la Coastal dhidi ya Shooting lilifungwa na kiungo wa zamani wa Simba, Haruna Moshi 'Boban' katika dakika ya 80

Vikosi kwenye Uwanja wa Taifa vilikuwa; Yanga: Ali Mustafa 'Barthez', Mbuyu Twite, David Luhende, Nadir Haroub 'Cannavaro', Kelvin Yondani, Athuman Idd 'Chuji', Simon Msuva, Frank Domayo, Didier Kavumbagu, Jerson Tegete/ Hamis Kiiza (dk 60), Haruna Niyonzima.

Azam: Aishi Manula, Erasto Nyoni, Waziri Salum, David Mwantika, Joackins Atudo/ Said Morad (dk 58), Himid Mao, Farid Musa/ Joseph Kimwaga (dk 72), Kipre Bolou, John Bocco 'Adebayor', Humphrey Mieno, Brian Umony/ Kipre Tchetche (dk 54).

TAKWIMU AZAM, YANGA
KONA: Azam 3, Yanga 3
MASHUTI: Azam 4 (Farid Musa dk 40, Kipre Balou 55, Joseph Kimwaga dk 82, 90), Yanga 11 (Kavumbagu dk 10, Twite dk 14 & 43, Msuva dk 27,49 na 89, Tegete dk 35 & 46, Domayo dk 63, David Luhende dk 80).

KUOTEA: Azam 5 (Bocco dk 27,42 & 77, Tchetche dk 76), Yanga 2 (Msuva dk 8, Tegete dk 53),
KADI YA NJANO: Kulikuwa kadi moja tu (ya njano) iliyotolewa kwa Atudo kwa kupoteza muda dk. 37
RAFU: Azam 8, Yanga 9
MABADILIKO: Azam 3, Yanga 1

Machapisho maarufu kutoka blogu hii

HISTORIA YA TIMU YA MASHUJAA YA KIGOMA, KUMBE NI SHEA YA JESHI NA WANANCHI

Timu inaitwa Mashujaa Lake Tanganyika FC ( Mashujaa FC ) ilianza rasmi kampeni yake ya kupanda Ligi Kuu tarehe 29/9/2018 na imepanda Ligi Kuu 25/06/2023 miaka mitano ya kupambana kwenye Ligi Daraja la kwanza Championship. Timu hii inaendeshwa kwa ushirikiano wa pande mbili kati ya Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) na Halmashauri ya Manispaa ya Kigoma Ujiji kwa niaba ya Wananchi wa Kigoma. Muelewe hapa maana wengi wanasema ni timu ya Jeshi asilimia 100% Nembo ya timu ni Sokwe Dume, Shujaa wa Hifadhi za Gombe na Mahale zilizopo mkoani Kigoma. Rangi ya kwanza ya jezi ya timu (first kit) ni hiyo hapo chini na kwenye nembo ya timu ni rangi za tunda la michikichi (mawese ). Hii kama njano ni mawese yaliyoganda na huo wekundu ni mawese ya moto. Ukishika tunda la Mse juu utaona wekundu na ukikata katikati utaona njano. Nyeupe ni ‘nazi’ ya Mse hizi ni alama za utajiri wa Kigoma Jezi nyingine ni blue inayowakilisha Ziwa Tanganyika na Jezi nyingine ni Nyeupe

MAKALA: SIMBA NI TIMU YA KWANZA TANZANIA KUINGIA NUSU FAINALI AFRIKA

Na Prince Hoza AFISA Habari wa klabu ya Yanga SC Ally Shabani Kamwe alidiriki kuudanganya umma wa wapenzi wa soka hapa nchini kwamba hakuna timu yoyote hapa Tanzania kuwahi kuingia hatua ya nusu fainali ya vilabu Afrika. Kamwe alisema timu yake ya Yanga itakuwa timu ya kwanza nchini kuingia nusu fainali ya Afrika, Yanga ilikuwa inakaribia kabisa kutinga nusu fainali ya kombe la Shirikisho barani Afrika. Yanga ilianza vizuri ikiwa ugenini baada ya kuilaza mabao 2-0 timu ya Rivers United ya Nigeria, hivyo ilikuwa inasubiria mchezo wa marudiano uliofanyika uwanja wa kumbukumbu ya Benjamin Mkapa jijini Dar es Salaam. Kwa vyovyote Yanga walikuwa na uhakika wa kutinga nusu fainali kwani walihitaji sare yoyote ama ushindi wa aina yoyote. Hapo ndipo Afisa Habari wa Yanga, Ally Kamwe aliamua kupiga vijembe kwa watani zake Simba SC na kuipotosha jamii kwa kudai kwamba Yanga itakuwa timu ya kwanza Tanzania kuingia nusu fainali ya Afrika. Kamwe ameifuta hadi rekodi ya Simba kuwa timu ya kwanza Tan...

Mabululu ni wa Simba SC

Simba wameweka donge nono kunasa saini ya mshambuliaji Agostinho Cristovan Paciencio Mabululu anayekipiga Al Tripoli ya Libya Ili ajiunge na Wekundu hao wa Msimhazi. Simba wamefanya mazungumzo ya moja kwa moja na wakala wa Mabululu na mchezaji mwenyewe na wako tayari kulipa kiasi cha juu zaidi kunasa saini ya mshambuliaji huyo hatari zaidi Simba wanahitaji kumalizana na mshambuliaji huyo badala ya kumaliza fainali ya kombe la Shirikisho, tayari Crecentius Magori yuko nyuma ya mpango huo kuhakikisha Simba ijayo inatisha. Mbali na Mabululu, Simba pia inahitaji Saini ya kiungo mshambuliaji wa Azam FC Feisal Salum "Feitoto" ambaye pia amewahi kuichezea Yanga SC