Ruka hadi kwenye maudhui makuu

BRANDTS AANZA VISINGIZIO, SIMBA NAO YAUFYATA KWA WANAJESHI ARUSHA

Kocha wa Yanga, Ernie Brandts (Pichani) ameelezea ushindani mgumu anaoutarajia katika mechi yao ya leo ya Ligi Kuu ya Bara dhidi ya Coastal Union kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam, huku Simba wakifanya mazoezi kwa kujificha mkoani Arusha kuelekea mechi yao ya leo dhidi ya JKT Oljoro.


Brandts alisema jana kuwa mechi ya leo kwenye Uwanja wa Taifa itakuwa ngumu kwa sababu Coastal imejiimarisha vyema katika kipindi hiki cha usajili tofauti na ilivyokuwa msimu uliopita.

"Coastal ni timu nzuri, wana wachezaji wazoefu, itakuwa mechi ngumu sana," alisema Mholanzi huyo, aliyeiongoza Yanga kutwaa ubingwa wa bara msimu uliopita baada ya kuikuta timu ikiwa mkiani mwa ligi baada ya kumfukuza aliyekuwa kocha wao Mbelgiji Tom Saintfiet.

Mkoani Arusha, Simba ilifanya mazoezi katika viwanja tofauti na nia ya kujificha kuelekea mechi yao ya leo.

Meneja wa timu hiyo ya Msimbazi, Mosses Basena, aliiambia NIPASHE hapa Arusha kwamba walilazimika kufanya mazoezi katika viwanja tofauti ili kujiweka mbali na hujuma zozote zinazoweza kufanywa dhidi yao.

Basena alisema kwa kuwa wako ugenini, lolote lingeweza kufanywa ili kuwadhoofisha katika mechi yao ya leo ndiyo maana walikuwa wakifanya mambo yao kwa kujificha.

Hata hivyo, Wekundu wa Msimbazi walifanya mazoezi katika uwanja wa Sheikh Amri Abeid jana asubuhi kama kanuni zinavyoagiza kwa wageni kujifua katika uwanja wa wenyeji siku moja kabla ya pambano.
Wachezaji kadhaa wa Simba walisema hawako tayari kuzungumza jambo lolote kuelekea mechi hiyo bila ya ruhusa maalum.

Simba inahitaji kushinda leo ili kujiweka sawa baada ya kulazimishwa sare ya 2-2 dhidi ya timu iliyopanda daraja ya Rhino Rangers ugenini Tabora katika mechi ambayo kocha Abdallah Kibadeni alimlalamikia kipa Mganda Abel Dhaira akisema alifungwa kizembe na kusema: "Tuna makipa watatu, tutaangalia mechi ijayo tutamchezesha yupi."

Mabingwa Yanga walianza ligi kwa kishindo wakitoa kipigo kikubwa zaidi cha siku ya ufunguzi baada ya kuishindilia timu iliyopanda daraja ya Ashanti kwa magoli 5-1 kwenye Uwanja wa Taifa, lakini hawatarajiwi kupata mteremko leo dhidi ya Coastal ambayo ina morali baada ya kuwafunga Oljoro kwa magoli 2-0 katika mechi yao ya kwanza.

Yanga na Coastal zitakutana kwenye Uwanja wa Taifa kuanzia saa 10.30 jioni kwa kiingilio cha Sh. 5,000, Sh. 8,000, Sh. 15,000 na Sh. 20,000 chini ya mwamuzi Martin Saanya wa Morogoro.

Katika mechi nyingine za leo, Mtibwa Sugar itaikaribisha Kagera Sugar kwenye Uwanja wa Manungu ulioko Turiani mkoani Morogoro wakati Uwanja wa Ali Hassan Mwinyi mjini Tabora utakuwa mwenyeji wa pambano kati ya wenyeji Rhino Rangers na Azam.

Vumbi lingine litatimka kwenye Uwanja wa Mabatini ulioko Mlandizi mkoani Pwani wakati maafande wa JKT Ruvu watakapokwaruzana na wenzao wa Tanzania Prisons kutoka Mbeya. Mbeya City na Ruvu Shooting zitacheza kwenye Uwanja wa Kumbukumbu ya Sokoine jijini Mbeya.

Jiji la Tanga litakuwa mwenyeji wa mechi kati ya Mgambo Shooting na Ashanti United itakayochezwa kwenye Uwanja wa Mkwakwani.

Machapisho maarufu kutoka blogu hii

HISTORIA YA TIMU YA MASHUJAA YA KIGOMA, KUMBE NI SHEA YA JESHI NA WANANCHI

Timu inaitwa Mashujaa Lake Tanganyika FC ( Mashujaa FC ) ilianza rasmi kampeni yake ya kupanda Ligi Kuu tarehe 29/9/2018 na imepanda Ligi Kuu 25/06/2023 miaka mitano ya kupambana kwenye Ligi Daraja la kwanza Championship. Timu hii inaendeshwa kwa ushirikiano wa pande mbili kati ya Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) na Halmashauri ya Manispaa ya Kigoma Ujiji kwa niaba ya Wananchi wa Kigoma. Muelewe hapa maana wengi wanasema ni timu ya Jeshi asilimia 100% Nembo ya timu ni Sokwe Dume, Shujaa wa Hifadhi za Gombe na Mahale zilizopo mkoani Kigoma. Rangi ya kwanza ya jezi ya timu (first kit) ni hiyo hapo chini na kwenye nembo ya timu ni rangi za tunda la michikichi (mawese ). Hii kama njano ni mawese yaliyoganda na huo wekundu ni mawese ya moto. Ukishika tunda la Mse juu utaona wekundu na ukikata katikati utaona njano. Nyeupe ni ‘nazi’ ya Mse hizi ni alama za utajiri wa Kigoma Jezi nyingine ni blue inayowakilisha Ziwa Tanganyika na Jezi nyingine ni Nyeupe

MAKALA: SIMBA NI TIMU YA KWANZA TANZANIA KUINGIA NUSU FAINALI AFRIKA

Na Prince Hoza AFISA Habari wa klabu ya Yanga SC Ally Shabani Kamwe alidiriki kuudanganya umma wa wapenzi wa soka hapa nchini kwamba hakuna timu yoyote hapa Tanzania kuwahi kuingia hatua ya nusu fainali ya vilabu Afrika. Kamwe alisema timu yake ya Yanga itakuwa timu ya kwanza nchini kuingia nusu fainali ya Afrika, Yanga ilikuwa inakaribia kabisa kutinga nusu fainali ya kombe la Shirikisho barani Afrika. Yanga ilianza vizuri ikiwa ugenini baada ya kuilaza mabao 2-0 timu ya Rivers United ya Nigeria, hivyo ilikuwa inasubiria mchezo wa marudiano uliofanyika uwanja wa kumbukumbu ya Benjamin Mkapa jijini Dar es Salaam. Kwa vyovyote Yanga walikuwa na uhakika wa kutinga nusu fainali kwani walihitaji sare yoyote ama ushindi wa aina yoyote. Hapo ndipo Afisa Habari wa Yanga, Ally Kamwe aliamua kupiga vijembe kwa watani zake Simba SC na kuipotosha jamii kwa kudai kwamba Yanga itakuwa timu ya kwanza Tanzania kuingia nusu fainali ya Afrika. Kamwe ameifuta hadi rekodi ya Simba kuwa timu ya kwanza Tan...

Mabululu ni wa Simba SC

Simba wameweka donge nono kunasa saini ya mshambuliaji Agostinho Cristovan Paciencio Mabululu anayekipiga Al Tripoli ya Libya Ili ajiunge na Wekundu hao wa Msimhazi. Simba wamefanya mazungumzo ya moja kwa moja na wakala wa Mabululu na mchezaji mwenyewe na wako tayari kulipa kiasi cha juu zaidi kunasa saini ya mshambuliaji huyo hatari zaidi Simba wanahitaji kumalizana na mshambuliaji huyo badala ya kumaliza fainali ya kombe la Shirikisho, tayari Crecentius Magori yuko nyuma ya mpango huo kuhakikisha Simba ijayo inatisha. Mbali na Mabululu, Simba pia inahitaji Saini ya kiungo mshambuliaji wa Azam FC Feisal Salum "Feitoto" ambaye pia amewahi kuichezea Yanga SC