Wakati
uongozi wa klabu ya Yanga ukiwa katika harakati za kutaka kumsajili
Mganda Moses Oloya anayecheza soka nchini Vietnam, uongozi wa Simba
ambayo pia inamuwania mshambuliaji huyo umesema utawapiga bao watani wa
jadi wao hao.
Akizungumza kwa njia ya
simu akiwa Nairobi, Kenya Mwenyekiti wa kamati ya usajili ya Simba,
Zacharia Hanspope alisema jana kuwa wanajua kuwa Yanga wanamfuatilia
mchezaji huyo lakini hawatishiki.
Alisema hawatishiki kwa kuwa wamefikia
hatua nzuri ya mzungumzo na mchezaji huyo anayemalizia mkataba wake
kwenye klabu yake ya huko Vietnam.
Hanspope alisema Simba haishindani na timu yoyote katika usajili na kwamba inafuata matakwa ya benchi la ufundi.
"Ni kweli sisi tunamfuatilia huyo mchezaji
na bado tupo naye kwenye mazungumzo ila kwa kiasi kikubwa tumekubaliana
vitu vingi," alisema mwenyekiti huyo.
"Kwa sasa kuna jambo moja tu tunalolisubiri ili kukamilisha taratibu zote."
Yanga imezoea kuingilia kati kila usajili
unaofanywa na Simba, alisema Hanspope, lakini safari hii timu yake ipo
makini kutorudia makosa waliyoyafanya msimu uliopita.
Simba iliporwa beki Mbuyu Twite wa APR
wakati huo licha ya kuwa ya kwanza kufanya naye mazungumzo, na
mwenyekiti Isamil Aden Rage kupiga naye picha nchini Rwanda, baada ya
Yanga kwenda kwa klabu mama ya mchezaji huyo ya FC Lupopo ya JK Kongo.
Alisema kuwa suala la usajili wa Oloya
wanaliendesha kwa umakini mkubwa kwa kuwa wanafahamu wenzao wanaweza
wakawatibulia na kushindwa kukamilisha usajili huo.
Wakati Hanspope akisema hivyo, Yanga
wanaendelea kusaka mchezaji mmoja wa kimataifa na taarifa zilizopo ni
kuwa yupo kiongozi aliyekwenda Vietnam kwa ajili ya kufanya mazungumzo
na kumalizana na mchezaji huyo.
Hata hivyo Mwenyekiti wa Kamati ya usajili ya klabu hiyo Abdallah bin Kleb alikataa kuzungumzia jambo hilo na kusema,
"Sitaki kuzungumzia jambo hilo kwa sasa
mpaka hapo mambo yatakapokamilika ila tunatafuta mshambuliaji mmoja wa
kimataifa," alisema bin Kleb.